1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dawa zilizopigwa marufuku zinachafua riadha

7 Agosti 2015

Wanariadha maarufu nchini Kenya wametoa wito kwa vyombo husika kuchukua hatua madhubuti za kupambana na tatizo la wanariadha kutumia dawa zilizopigwa marufuku michezo

https://p.dw.com/p/1GBlC
40. Berlin-Marathon Wilson Kipsang Kiprotich 29.09.2013
Picha: picture-alliance/dpa

Wanariadha maarufu nchini Kenya wametoa wito kwa shirikisho la riadha la kitaifa, shirikisho la riadha la kimataifa – IAAF na shirikisho la kimataifa la kupambana na matumizi ya dawa zilizopigwa marufuku michezoni – WADA kuchukua hatua kuhusiana na ripoti za kuongezeka matukio ya matumizi ya dawa za kuongeza nguvu mwilini.

Aliyekuwa mshikilizi wa rekodi ya ulimwengu ya mbio za marathon Wilson Kipsang, ambaye pia ni mwenyekiti wa Chama cha Wanariadha wa Kulipwa nchini Kenya amesema ripoti kuwa zaidi ya wanariadha 800, wakiwemo Wakenya 18 walikuwa na matokeo ya kutiliwa shaka ya vipimo vya damu baina ya mwaka wa 2001 na 2012 zinaharibu sifa ya mchezo huo "Suala la matumizi ya dawa zilizopigwa marufuku ni kubwa na unapojaribu kuona Chama cha Riadha Kenya nadhani hawafanyi vya kutosha linapokuja suala la uhamasishaji na kuhakikisha kuwa hatua za udhibiti zinachukuliwa, kwa sababu wanariadha wengi hawafahamu ni dawa zipi na namna ya kuziepuka, hivyo nadhani mengi yanastahili kufanywa".

Kipsang amesema madai hayo hayatawahofisha wanariadha wa Kenya wakati wakijiandaa kwa mashindano ya ubingwa wa dunia yanayoanza mjini Beijing baadaye mwezi huu. Wakenya pia wanawalaumu wakufunzi wa kigeni wanaoingia nchini humo. Mshindi wa zamani wa mbio za New York Marathon Tegla Loroupe anasema serikali ya Kenya inapaswa kuwadhibiti wageni wanaoingia nchini humo kuwapa mafunzo wanariadha.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/Reuters
Mhariri: Iddi Sessanga