1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Msako wa washambuliaji wa Charlie Hebdo waendelea

Amina Abubakar8 Januari 2015

Polisi wa Ufaransa wanaendelea kuwasaka watu wawili wanaowashuku kwa mashambulizi dhidi ya ofisi za jarida la Charlie Hebdo yaliyouwa watu 12, huku baadhi ya taasisi za Kiislamu zikishambuliwa.

https://p.dw.com/p/1EGaL
Washukiwa wawili wa Ugaidi,Cherif Kouachi na Said Kouachi
Washukiwa wawili wa Ugaidi,Cherif Kouachi na Said KouachiPicha: picture-alliance/dpa/French Police/Handout

Hali ya wasiwasi imezidi kutanda nchini Ufaransa huku serikali ikitangaza leo kuwa siku ya maombolezo baada ya mauaji hayo ya jana. Waziri Mkuu wa Ufaransa, Manuel Valls, amesema washukiwa wa mashambulizi hayo wametambuliwa na maafisa wa ujasusi kuwa ni ndugu wawili, Cherif na Said Kouachi.

Cherif, mwenye umri wa miaka 32, anatuhumiwa pia kwa kukusanya wapiganaji wa jihadi kwa ajili ya kwenda Iraq na pia kukutwa na mwaka 2008 alikutwa na hatia ya ugaidi.

“Yeye pamoja na kaka yake wanapaswa kuchukuliwa kama watu hatari," ilisema polisi ya Ufaransa.

Polisi kusini mwa Ufaransa wakimsaidia mwenzao aliyeshambuliwa na watu waliokuwa kwenye gari mapema Alhamisi, tarehe 8 Junuari 2015.
Polisi kusini mwa Ufaransa wakimsaidia mwenzao aliyeshambuliwa na watu waliokuwa kwenye gari mapema Alhamisi, tarehe 8 Junuari 2015.Picha: Reuters/C. Platiau

Msemaji wa Ofisi ya Mwendesha Mashitaka mjini Paris, Agnes Thibault-Lecuivre, amesema mshukiwa wa tatu, Mourad Hamyd, mwenye umri wa miaka 18, amejisalimisha mwenyewe polisi katika kijiji kimoja mashariki mwa Ufaransa, baada ya kugundua kuwa jina lake lilikuwa miongoni mwa washukiwa wa mashambulizi waliotangazwa katika mitandao ya kijamii na hata vyombo vya habari.

Hata hivyo, Agnes hakusema mshukiwa huyo alikuwa na mahusiano ya aina gani na kaka hao wawili wanaodaiwa kuhusika na mauaji ya jana.

Hali ya hadhari yaimarishwa

Kwa sasa Ufaransa imeongeza tahadhari dhidi ya ugaidi na kuimarisha usalama kwenye maeneo kadhaa, ambapo zaidi ya wanajeshi 800 wanashika doria katika ofisi tofauti za vyombo vya habari, maeneo ya kuabudu, maeneo ya usafiri na maeneo mengine yaliyoko katika hatari ya kushambuliwa.

Kumekuwa na taarifa za misikiti kushambuliwa na makundi ya waandamanaji wanaodai kulipiza kisasi mauaji ya jana.

Bendera ikipepea nusu mlingoti nchini Ufaransa baada ya mashambulizi dhidi ya ofisi za gazeti la Charlie Hebdo.
Bendera ikipepea nusu mlingoti nchini Ufaransa baada ya mashambulizi dhidi ya ofisi za gazeti la Charlie Hebdo.Picha: Reuters/P. Wojazer

Kumekuwa pia na taarifa za mashambulizi mengine dhidi ya polisi kusini mwa Ufaransa, ambako watu waliokuwa kwenye gari wamewapiga risasi polisi wawili na kumuua mmoja wa kike. Hakuna ushahidi wa kuyaunganisha matukio mawili hayo hadi sasa.

Huku hayo yakiarifiwa raia nchini Ufaransa wanatarajiwa kunyamaa kimya kwa dakika moja mchana wa leo ili kuwakumbuka wahanga wa mashambulizi ya hapo jana, ambapo waandishi wanane wa habari, maafisa wawili wa polisi, mfanyakazi mmoja na mgeni aliyetembelea ofisi hiyo waliuwawa.

Dunia yaungana na Ufaransa

Kwa upande mwengine, viongozi kadhaa duniani wameendelea kulaani mashambulizi hayo. Rais Barrack Obama wa Marekani amesema nchi yake itasimama na Ufaransa katika wakati huu mgumu, huku Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, akisema mashambulizi hayo "yanaiingilia demokrasia na uhuru wa vyombo vya habari."

Waandamanaji wakiwakumbuka wahanga wa mashambulizi dhidi ya ofisi za gazeti la Charlie Hebdo.
Waandamanaji wakiwakumbuka wahanga wa mashambulizi dhidi ya ofisi za gazeti la Charlie Hebdo.Picha: DW/A. Mohtadi

Naye Waziri Mkuu wa Australia, Tony Abbott, ameyalaani mashambulizi hayo na kuyaelezea kama kitendo cha ukatili wa hali ya juu, huku Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameroon akisema Uingereza iko pamoja na Ufarasa dhidi ya ugaidi na dhidi ya kitisho cha maadili wanayoyalinda, uhuru wa kujieleza pamoja na demokrasia.

Mwandishi: Amina Abubakar/AFP/Reuters
Mhariri: Iddi Ssessanga