1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WASHINGTON: Kikosi maalumu cha jeshi la Marekani chaingia Somalia

12 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCbQ

Gazeti la Washington Post limeripoti katika toleo lake la leo kwamba kikosi maalumu cha jeshi la Marekani kimeingia Somalia kufuatia shambulio la angani kusini mwa nchi hiyo mapema wiki hii.

Likizinukulu duru zisizojulikana, gazeti hilo limesema wanajeshi wameingia kusini mwa Somalia kutathmini waliouwawa katika shambulio hilo.

Walengwa wa shambulio hilo walikuwa viongozi wa al-Qaeda wanaotuhumiwa kupanga mashambulio dhidi ya balozi za Marekani nchini Kenya na Tanzania mnamo mwaka wa 1998.

Balozi wa Marekani nchini Kenya amekanusha habari kwamba viongozi hao wa al-Qaeda waliuwawa katika shambulio la kusini mwa Somlia. Watu kumi, wakiwemo washukiwa wa ugaidi waliuwawa katika shambulio hilo la angani lililofanwa na wanajeshi wa Marekani kusini mwa Somalia.

Wakati haya yakiarifiwa, kiongozi wa ujasusi nchini Marekani, John Negroponte, amesema viongozi wa al-Qaeda wamepata maficho nchini Pakistana ambako wanajiimarisha.

Aidha Negroponte amesema wapiganaji wa al Qaeda wanajiimarisha katika eneo la Mashariki ya Kati, kaskazini mwa Afrika na barani Ulaya.