1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaChina

Wataalamu: Huenda kukazuka kirusi kipya cha Corona

29 Desemba 2022

Wataalamu waonya huenda kukazuka aina mpya ya kirusi cha Corona katika wakati huu ambao China inashuhudia kiwango kikubwa cha maambukizi katika mwezi huu, na hivi karibuni ikiondoa masharti ya kuthibiti kuenea kwa Uviko.

https://p.dw.com/p/4LW4X
Das Leben in ehemaligen Pandemie-Hotspots heute
Picha: DW

Wakati onyo hilo likitolewa baadhi ya mataifa ikiwemo Marekani yametangaza masharti mapya kwa wasafiri kutoka China.

Katika wiki tatu za kwanza za mwezi Desemba pekee, inakadiriwa watu milioni 248 nchini China waliambukizwa virusi hivyo.

Huku hospitali na sehemu za kuchomea maiti zikielemewa,katika taifa hilo ambalo hivi karibuni mamlaka ilitangaza kusitisha sera yake ya udhibiti wa maambukizi iliokuwepo tangu kuzuka kwa janga hilo miaka mitatu iliopita.

Wataalamu wa masuala ya afya wanahofia kwamba China itakuwa ni kitovu cha kuzalisha aina mpya ya virusi, ambapo hadi sasa vinaweza kusambaa miongoni mwa karibu moja ya tano ya watu duniani ambao hawana kinga ya kutosha na wale ambao hawajachanjwa.

Soma pia: Maambukizi ya COVID-19 duniani yapindukia milioni 400

Antoine Flahault, mkurugenzi wa Taasisi ya Afya Ulimwenguni katika Chuo Kikuu cha Geneva, ameliiambia shirika la habari la AFP kwamba kila "maambukizo mapya yanaongeza nafasi ya virusi kubadilika."

Hoja hiyo inaunga mkono na Soumya Swaminathan, ambaye aliwahi kuwa mwanasayansi mkuu wa Shirika la Afya Ulimwenguni hadi mwezi Novemba, akisema mtu kutopata chanjo hasa kwa makundi ya wazee kunaongeza hatari.

"Sehemu kubwa ya Wachina wako katika hatari ya kuambukizwa sababu wazee wengi hawajachanjwa au kupata chanjo ya nyongeza."

 Amesisitiza kwa sasa kuna haja ya kuwa makini na aina nyingine za virusi itakavyojitokeza.

Masharti mapya kwa wasafiri kutoka China

Katika kuchukua hatua ya kudhibiti maambukizi hayo yanayoshuhudiwa kuongezeka, baadhi ya mataifa ikiwemo Marekani, Italia, Japan, India na Malaysia, mapema wiki hii yametangaza mashart ya kiafya kwa wasafiri wanaoingia wakitokea China pamoja na maeneo yake maalum ya utawala ya Hong Kong na Makau.

Waziri mkuu wa Australia Anthony Albanese amesema wanatekeleza ushauri wa wataalamu wa afya kwa kuhakikisha kila mmoja anapima kabla ya kuingia nchini humo.

Soma pia: Corona yaendea kuitikisa dunia

"Tunachokifanya ni kuchukua hatua sio tu kwa sababu ni China." Alisema waziri huyo mkuu huyo na kuongeza kwamba watafuata ushauri wa wataalamu katika kujiondoa kwenye hatari.

"Watu watapaswa kupima kabla ya kupanda ndege, hivyo kuna hatua mbalimbali tutazichukua."

Vituo vya udhibiti wa magonjwa nchini Marekani navyo vimetangaza hatua hiyo itakayoanza kutekelezwa kuanzia januari 5, ambapo wasafiri watalazimika kutoa taarifa zao za vipimo na chanjo dhidi ya corona kabla ya kuondoka.

India na Japani nazo zinatekeleza sharti la upimaji wa lazima wa kipimo cha PCR kwa abiria wote kutoka China, ikiwa ni njia moja wapo itakayosaidia, iwapo kuna uchaleweshwaji wa taarifa kutoka Beijing.wataalamu wameshauri.

Mkuu wa taasisi ya kudhibiti virusi katika Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa China Xu Wenbo aliwaambia waandishi wa habari kwamba aina nyingine ndogo za Omicron zimegunduliwa hivi karibuni nchini China katika kipindi cha miezi mitatu iliopita.