1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wataalamu waonya kuhusu mabadiliko ya tabia nchi

31 Machi 2014

Watalaamu wa mambo ya hali ya hewa wanasema athari za mabadiliko ya tabia nchi tayari zinatokea katika mabara yote na baharini, na ulimwengu haujajiandaa kupambana na hatari inayosababishwa na mabadiliko hayo

https://p.dw.com/p/1BYpt
Bildergalerie Mutterliebe
Picha: picture alliance/Photoshot

Jopo la Kimataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabia Nchi – IPCC linaloungwa mkono na Umoja wa Mataifa limekamilisha ripoti yake kuhusu athari za mabadiliko ya tabia nchi kwa maisha ya binaadamu na mfumo asilia wa mazingira ya dunia, pamoja na mbinu zinazoweza kutumiwa kukabiliana na hali hiyo. Mkutano wa wataalamu hao ulifanyika wiki iliyopita katika mji wa Yokohama nchini Japan.

Ripoti hiyo inasema athari za majanga ya karibuni yanayohusiana na hali ya hewa, kama vile ongezeko la joto kali,ukame, mafuriko, vimbunga na moto wa misituni zinadhihirisha hatari kubwa iliyopo kwa binaadamu na mifumo ya asili.

Vicente Barros, mwenyekiti msaidizi kwa jopo hilo linalowajumuisha mamia ya wanasayansi na wawakilishi wa serikali, amesema ulimwengu unaishi katika enzi ya mabadiliko ya tabia nchi yanayosababishwa na binaadamu.

Mabadiliko ya tabia nchi ni kitisho kinachoongezeka kwa usalama wa binadamu kwa sababu yanasababisha uharibifu kwa makaazi na mali, yanavuruga upatikanaji wa chakula na maji na kushurutisha watu kuzihama sehemu zao za asili.

Wanasayansi wanaonya kuwa raslimali kama vile maji na chakula, zinaanza kuwa adimu
Wanasayansi wanaonya kuwa raslimali kama vile maji na chakula, zinaanza kuwa adimuPicha: AFP/Getty Images

Mwenyekiti wa jopo hilo la IPCC Rajendra Pachauri amewaambia waandishi wa habari leo kuwa hakuna yeyote duniani ambaye atanusurika kutokana na athari za mabadiliko ya tabia nchi. Hatari ya mabadiliko ya tabia nchi yatakuwa ya kiwango cha “juu hadi kupindukia” iwapo joto litaongezeka zaidi ya nyuzijoto nne juu ya viwango vya kabla ya ustawi wa kiviwanda, ambako ulimwengu sasa unaelekea.

Pachauri anasema kitu muhimu walichoafikiana ni kuhusu umuhimu wa kuwa na mbinu za kuweza kukabiliana na hali hiyo kwa sababu ndiyo njia pekee ambayo ulimwengu unaweza kupunguza hatari ya mabadiliko ya tabia nchi. Ripoti hiyo inasema wazi kuwa bado upo muda wa kuchukua hatua. Samantha Smith kutoka Shirika la mfuko wa kutunza mazingira ya dunia, World Wide Fund for Nature Campaign hata hivyo anasema bila hatua madhubuti na za haraka, dunia inakabiliwa na kitisho cha kufika mahali ambako itakuwa haina la kufanya kuhusu hali hii ya mabadiliko ya tabia nchi.

Mnamo mwezi Septemba mwaka jana, jopo la IPCC lilionya kuwa binaadamu ndio kimsingi wanaosababisha ongezeko la joto duniani, ambalo limesababisha kuongezeka kwa kina cha bahari kwa kiwango ambacho hakikufikiriwa hapo awali, na kuyeyuka barafu kwa kasi.

Ripoti ya tatu itakayoangazia mbinu za kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi itazinduliwa mwezi wa Aprili mjini Berlin. Mkutano wa kilele mjini Paris mwaka wa 2015 utaangazia kuundwa kwa mkataba mpya wa kimataifa kuhusu hali ya hewa, ili kuchukua nafasi ya muafaka wa Kyoto wa mwaka wa 1997, ambao awamu ya kwanza ilikamilika mwishoni mwa mwaka wa 2012.

Mwandishi: Bruce Amani/DPA
Mhariri: Daniel Gakuba