1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watoto waendelea kufanyishwa kazi duniani

12 Juni 2012

Leo(12.06.2012) ni siku ya kimataifa ya kupambana na ajira dhidi ya watoto ambapo watoto milioni 215 wanafanyishwa kazi, nusu yao katika mazingira hatari kwa mujibu wa Shirika la Kazi Duniani (ILO).

https://p.dw.com/p/15CeA
Wer hat das Bild gemacht?: Yaya Boudani Wann wurde das Bild gemacht?: Anfang Juni 2012 Wo wurde das Bild aufgenommen? :Burkina Faso
Watoto wanaofanyakazi katika migodi Burkina FasoPicha: DW

Watoto hawa hufanyishwa kazi katika machimbo ya dhahabu, wanatupa taka kutoka katika majumba ya watu wengine, ama wanasuka mazulia katika viwanda. Watoto hawa hawawezi kuandika hata jina lao, ama kusoma kitabu, kucheza kwao ni jambo ambalo halimo katika msamiati wao.

Zenabou Ilboudou ni dada mkubwa. Sio katika hali halisi, hapana, dada huyu mwenye umri wa miaka 20 anafanyakazi katika wakfu wa Terre des Hommes , kama dada mkuu, kwa wasichana, ambao wamekuwa wakifanyishwa kazi kama wafanyakazi wa ndani. Kwasababu Zenabou Ilboudou anafahamu tatizo hili, kwa kuwa aliwahi binafsi kwa muda wa miaka saba kufanyakazi kama mfanyakazi wa nyumbani katika mji mkuu wa Burkina Faso, Ouagadougou. Wakati akianza kazi hiyo alikuwa na umri wa miaka tisa.

Wer hat das Bild gemacht?: Yaya Boudani Wann wurde das Bild gemacht?: Anfang Juni 2012 Wo wurde das Bild aufgenommen? :Burkina Faso
Wasichana wakifanyakazi za nyumbani Burkina FasoPicha: DW

"Asubuhi saa kumi na moja anakuamsha mama mwenye nyumba , ili uanze kazi za ndani, na ananipa pesa kwa ajili ya kununulia vyakula vya nyumbani. Baada ya hapo hupika , na wakati baba mwenyenyumba hatapendelea mchuzi uliotengeneza , unaingia katika matatizo. Iwapo hutapigwa, utagombezwa na kutukanwa. Mchana kupata chakula ni taabu. Sehemu yako ya kulala mara nyingi ni jikoni ama sakafuni".

Familia hukosa uwezo wa kujiendesha

Nchini Burkina Faso pamoja na nchi nyingine za Afrika kuna maelfu kadha ya wafanyakazi wa nyumbani ambao wamefikwa na madhila yaliyomfika Zenabou Ilboudou. Wengi wao wako katika umri kati ya miaka 9 na 14, wakati walipoanza kutafuta kazi. Wengi wao wanakimbia kutoka katika familia zao kwasababu kwao wazazi wao hawana fedha, ama wameuzwa. Masharti ya kazi kwa kiasi kikubwa ni kinyume na ubinadamu, watoto wanatumiwa kama watumwa, hupigwa, hufanyiwa mambo mabaya, ama kudhalilishwa kingono.

Ahadi za uongo

Halima Fogo hivi sasa ana umri wa miaka 21. Alikuwa kwa muda wa miaka sita akifanyakazi kama mfanyakazi wa nyumbani na amekuwa akidhalilishwa kingono mara kwa mara na waajiri wake wanaume.

"Wakati baba mwenye nyumba akitoka kazini na kurudi nyumbani, kwa kuwa mke wake hayuko nyumbani, anaanza. Hunipa vishawishi, na kusema , iwapo nitalala nae , mwishoni mwa mwezi ataniongezea mshahara".

Terre des hommes: Kinderhilfe zu Kinderarbeit in Burkina Fas© Tdh | R. Rorandelli***ACHTUNG: Das Bild darf ausschließlich im Rahmen einer Berichterstattung (über Terre des hommes) genutzt werden***
Msichana wa kazi Burkina FasoPicha: Tdh | R. Rorandelli

Ni vishawishi ambavyo ni kinyume na ubinadamu, ni ahadi za uwongo. Zaidi ya hayo, sehemu kubwa ya watoto wanaofanyishwa kazi, kiasi ya theluthi moja , hata hivyo hupata sehemu ndogo ya mshahara wao, ama hawapati kabisa.

Serikali inafanya juhudi

Wengi wao wanafanyakazi katika kile kinachoitwa sekta isiyo rasmi., katika sekta hii hakuna mkataba ama mafao ya kijamii.

Wakati huo huo, serikali ya Burkina Faso inatambua matatizo haya na inajaribu kubadilisha mwelekeo huo, kwa kushirikiana na mashirika kadha ya kijamii nchini humo, na hata pia mashirika ya kimataifa kama Terre des Hommes ama Unicef. Na hii inahusu kuzuwia utumwa, kuwatumia watoto katika biashara ya ngono, kuwatumia watoto kama wanajeshi na kuwatumia watoto katika kazi za hatari.

Herman Zoungrana , meneja mradi wa Terre des Hommes nchini Burkina Faso, anaelezea kile shirika hilo inachokifanya.

"Kwa hivi sasa tuna mpango unaowahusu wasichana 700, ambao wameweza kwenda shule katika vijiji wanakotoka, pamoja na mradi wa mafunzo ya kazi unaowahusu karibu wasichana wengine 100. Wanafanyakazi kwa mfano katika mikahawa ama viwanda vidogo vya kushona. Na wengine zaidi ya 100 wanasoma katika shule ya sekondari katika mji wa Tougan, kaskazini magharibi ya Burkina Faso".

Kazi ya migodini

Hata hivyo, kwa bahati mbaya hili ni tone tu linalodondoka katika jiwe lenye joto. Zaidi ya watoto 500,000 wanafanyishwa kazi linasema shirika la kazi la kimataifa nchini Burkina Faso. Na hii sio tu katika majumba ya watu binafsi. Karibu nusu wanafanyakazi katika takriban machimbo 600 ya dhahabu nchini humo. Mikono midogo ya vijana hawa hutumika kuvunja vunja mawe ili kuweza kupata dhahabu. Miili midogo ya vijana hawa hutumika kupenya katika mashimo madogo ya machimbo ya dhahabu. Mapafu yao huvuta hewa chafu ya kemikali zenye sumu za sianidi , ama kemikali za asidi salfuriki. Malipo kwa watoto hawa ni ya shida, hupewa chakula tu. Zenabou Dipama mwenye umri wa miaka 15 ana mikono mikubwa kutokana na kuvunja mawe.

Wer hat das Bild gemacht?: Yaya Boudani Wann wurde das Bild gemacht?: Anfang Juni 2012 Wo wurde das Bild aufgenommen? :Burkina Faso
Mtoto mdogo akivunja mawe katika mgodi wa dhahabu Burkina FasoPicha: DW

"Tumeajiriwa wanawake kwa ajili ya kubeba mawe na kuyavunjavunja. Ni kazi ngumu, ngumu sana".

Sayouba Bonkoungou, mwenye umri wa miaka 15, pia anafanyakazi hapa pia.

"Muda wa kisheria wa kufanyakazi hapa hakuna. Tunaanza tangu asubuhi , mchana tunapumzika kidogo na baada ya hapo kazi inaendelea hadi usiku wa manane".

Wer hat das Bild gemacht?: Yaya Boudani Wann wurde das Bild gemacht?: Anfang Juni 2012 Wo wurde das Bild aufgenommen? :Burkina Faso
Mgodi wa dhahabu Burkina FasoPicha: DW

Shule nyingi katika eneo lenye machimbo ya dhahabu zina wanafunzi wachache. Watoto wameamua kuwa hawana muda wa kwenda shule. Shirika la umoja wa mataifa ya kuwahudumia watoto, UNICEF, hata hivyo limefanikiwa kuwapeleka watoto 7,000 shuleni na hii ni hali ya kutia moyo. Na mafanikio haya si rahisi kila mara. Kwasababu kazi katika machimbo ya dhahabu inawavutia watoto wengi licha ya ugumu wake.Wanafikiria kufanyakazi ya kuvunja mawe na kupata dhahabu kidogo ili kupambana na umasikini unaowakabili.

Mwandishi : Köpp, Dirke, Boudani, Yaya / ZR / Sekione Kitojo

Mhariri: Miraji Othman