1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wazanzibari wakubali kuundwa kwa serikali ya Umoja wa Kitaifa

Josephat Nyiro Charo1 Agosti 2010

Ni shangwe na nderemo kwa wale waliounga mkono mageuzi ya katiba yatakayowezesha kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa Zanzibar baada ya uchaguzi mkuu Oktoba 31 mwaka huu

https://p.dw.com/p/OZLt
Rais wa Zanzibar, Aman Abeid KarumePicha: AP Photo

Wazanzibari wamekubali kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa kufuatia matokeo ya kura ya maoni yaliyotangazwa leo na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar katika hafla iliyohudhuiriwa na wadau mbalimbali wakiwemo mabalozi wa nchi za nje na vyama vya siasa mjini Zanzibar.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) Bw. Khatib Mwinyichande, kura ya ndio imeongoza kwa asilimia 66.4 huku kura ya hapana ikipata asilimia 33.6. kati ya kura zote zaidi ya laki mbili zilizopigwa jana.

Matokeo hayo yanaruhusu mageuzi ya katiba kuviwezesha vyama vya kisiasa kuunda serikali ya mseto itakayomaliza uhasama wa kisiasa huko Zanzibar, ambayo ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kura hiyo ya maoni ilifanyika kwa amani katika visiwa vya Ugunja na Pemba na serikali ya umoja wa kitaifa inatarajiwa kuundwa baada ya uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 31 mwaka huu.