1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Clinton asema ujenzi siyo halali!

Abdu Said Mtullya4 Novemba 2009

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Hillary Clinton amesema ujenzi wa makaazi ya walowezi siyo halali.

https://p.dw.com/p/KOah
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Hillary Clinton.Picha: picture alliance / abaca

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Hillary Clinton amesema ujenzi wa makaazi ya walowezi wa kiyahudi siyo halali, lakini amesema anaamini kuanzishwa tena mazungumzo ya amani ndiyo itakuwa njia ya haraka ya kufikia kwenye lengo la kusimamisha ujenzi wa makaazi hayo.

Waziri Clinton amesema leo mjini Cairo kwamba Marekani haikubaliani na ujenzi wa makaazi hayo. Ameeleza kuwa Marekani inaamini kuwa ujenzi wa makaazi siyo jambo halali. Amesisitiza kwamba hiyo ndiyo imekuwa sera ya serikali ya nchi yake katika kipindi cha miaka 40 iliyopita.Waziri Clinton ametamka kuwa hiyo ndiyo sera ya rais Obama leo na itaendelea kuwa hivyo.

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Clinton alisema hayo baada ya kukutana na rais Hosni Mubarak wa Misri mjini Cairo mapema leo. Waziri huyo amesema litakuwa jambo la munufaa ikiwa shughuli za ujenzi wa makaazi ya walowezi zitaachwa sasa na katika siku za usoni.

Hatahivyo amesisitiza kwamba kuingia katika hatua za mwisho za mazungumzo kutawezesha kukomeshwa kwa ujenzi wa maakazi hayo.

Akizungumzia juu ya suala hilo, naye waziri wa mambo ya nje wa Misri, Ahmed Gheit amesema ni msimamo wa nchi yake kwamba pana haja ya kuelekeza juhudi katika kufikia suluhisho badala ya kupoteza wakati na kukwama juu ya suala la ujenzi wa maakazi. Waziri Gheit amesema mazungumzo lazima yaanzishwe tena .

Nchi za kiarabu zilivunjika moyo hapo awali baada ya waziri wa mambo ya nje wa Marekani Clinton kuafikiana na msimamo wa Israel kwamba suala la ujenzi halipaswi kuzuia hatua ya kuanzisha tena mazungumzo ya amani.

Viongozi wa Palestina hapo awali walisema walikuwa wanahofia kwamba serikali ya Israel ilikusudia kufanya mazungumzo kama njama za kuiliwaza jumuiya ya kimataifa ili ipate wakati wa kuendelea na ujenzi wa makaazi ya walowezi.

Rais Mubarak wa Misri pia amesisitiza kwamba wapalestina wana haki ya kudai kupewa uhakika.

Wakati huo huo mjumbe wa kimataifa wa wapalestina Saeb Erekat amesema mjini Ramallah leo , kwamba rais wa mamlaka ya Palestina Mahmoud Abbas hatasimama tena katika uchaguzi ikiwa hapatakuwa na dalilili za dhati za mazungumzo ya amani na Israel.

Rais Mahmoud Abbas anahesebakika kuwa kiongozi mwenye mzatamo wa ukadirifu.

Hatahivyo waziri wa mambo ya nje wa Marekani Hillary Clinton amesema leo mjini Cairo kuwa suala la mji wa Jerusalem pia lazima lihusishwe katika mazungumzo.

Mwandishi/Mtullya Abdu.

Mhariri/Abdul-Rahman.