1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri Mkuu Maliki aongoza katika uchaguzi wa Iraq

Prema Martin8 Machi 2010

Waziri Mkuu wa Iraq, Nuri al-Maliki, aliyesaidia kutuliza mizozo ya kimadhehebu nchini Iraq, anashika nafasi ya mbele katika uchaguzi unaotazamwa kama mtihani wa demokrasia changa nchini humo.

https://p.dw.com/p/MMuH
Iraq's Prime Minister Nouri al-Maliki speaks during the opening ceremony of a new airport in Najaf, south of Baghdad, Iraq, 20 July 2008. EPA/HUSSEIN AL-MOUSAWI +++(c) dpa - Bildfunk+++
Waziri Mkuu wa Iraq Nuri al-Maliki.Picha: picture-alliance/ dpa
Matokeo rasmi ya mwanzo yanatazamiwa kutangazwa katika kipindi cha siku chache zijazo. Muungano wa vyama vya Kishia,"State of Law Coalition" unaoongozwa na Waziri Mkuu al-Maliki unadai kuwa upo njiani kujinyakulia ushindi katika eneo la Baghdad na katika wilaya zingine kusini mwa nchi wanakoishi Washia wengi zaidi. Hata hivyo, Nur al-Maliki anakabiliwa na changamoto kali kutoka washirika wake wa zamani wa Kishia waliounda chama cha "Iraqi National Alliance" (INA), kinachodhibitiwa na vyama viwili vikuu vya Kishia.

Wakati huo huo chama cha waziri mkuu wa zamani, Iyad Allawi, kinachotenganisha dini na siasa, kinashika nafasi ya tatu. Chama hicho kinaungwa mkono na Wairaqi wengi wa madhehebu ya Kisunni ambao ni wachache na wamepoteza ushawishi katika serikali ya al-Maliki inayodhibitiwa na Washia walio wengi.

Iraqi president Jalal Talabani heads a meeting of various political parties of Iraq, in Baghdad, Iraq, Tuesday, March 14, 2006. Leaders of Iraq's main ethnic and religious blocs began a series of marathon meetings Tuesday in an attempt to break the deadlock. U.S. Ambassador Zalmay Khalilzad, who has been shuttling between the main factions, joined the session hosted by Shiite leader Adbul-Aziz al-Hakim. (AP Photo/Karim Kadim)
Rais wa Iraq, Jalal Talabani.Picha: AP

Na katika eneo la Wakurdi, kaskazini mwa Iraq, chama kipya kilichoundwa na mpenda mageuzi, Goran, kinashindana na chama cha PUK cha Rais Jalal Talabani. Kundi hilo jipya huenda likapunguza nguvu za PUK na KDP vilivyodhibiti katika uwanja wa kisiasa wa Wakurdi tangu miongo kadhaa. Katika siku zilizopita, mshikamano wa vyama hivyo ulisaidia kuwapa sauti Wakurdi katika siasa za Iraq.

Hivi sasa nchini Iraq, kwa sehemu kubwa, makundi yaliyokuwa yakiwakilisha jamii kwa ukabila na dini yamesambaratika. Baadhi ya makundi hayo yamevuka mipaka ya kidini na upo uwezekano wa makundi hayo kuanzisha majadiliano ya kuunda serikali mpya ya muungano, ikiwa hata chama kimoja hakitojinyakulia wingi katika bunge lenye viti 325. Majadiliano kama hayo ni mtihani kwa demokrasia dhaifu nchini Iraq, huku Marekani ikitazamia kupunguza kwa nusu idadi ya wanajeshi wake na kusitisha operesheni za kijeshi ifikapo tarehe 31 mwezi Agosti.Rais wa Marekani, Barack Obama, ameazimia kuwarejesha nyumbani wanajeshi wote wa Marekani kutoka Iraq ifikapo mwisho wa mwaka 2011.

Maafisa wa Marekani wanasema mpango huo unaweza kuhatarishwa, ikiwa tu hali ya usalama itadhoofika nchini Iraq. Kwa maoni ya mtaalamu David Mack wa Taasisi ya Mashariki ya Kati, katika nchi kama Iraq haitoshi kushinda uchaguzi tu, kinachohitajiwa ni uongozi wenye ufanisi.

Mwandishi: Prema Martin/Reuters/AFP

Mhariri: Miraji Othman