1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wiki moja Unusu zaidi kusalimisha silaha Basra

Kalyango Siraj28 Machi 2008

Waziri mkuu aahidi kutoa pesa kwa wapiganaji watakao salimisha silaha zao

https://p.dw.com/p/DWXB
Wapiganaji wa Kishia watiifu kwa kiongozi wa kidini mwenye msimamo mkali Moqtada al-Sadr wakiwa na silaha zao mjini Basra, kusini mwa Iraq tarehe 27 March 2008.Mapigano kati ya vikosi vya serikali na wapiganaji wa jeshi la Mahdi yanaendelea.Waziri mkuu ameahidi kutoa pesa kwa watakaosalimisha silaha zao kwa wanausalamaPicha: picture-alliance/ dpa

Bunge la Iraq limepangiwa kukutana leo ili kujadili hali ya usalama nchini humo kufuatia kuongezeka kwa mapigano kati ya vikosi vya serikali na vya Marekani dhidi ya wapiganaji wa kishia katika miji ya Baghadad na Basra.

Mapigano yalianza wakati utawala wa Iraq ulipoanzisha operesheni ya kuyanyanganya magenge yenye silaha katika mji wa kusini mwa nchi hiyo ambao una utajiri wa mafuta.Kiongozi wa kudini mwenye msimamo mkali Moqtadar al-Sadr anasema operesheni hiyo ililengwa kwa vijana wake wa jeshi la Mahdi.

Serikali ya Iraq imetangaza amri ya kutotembe usiku hadi jumapili asubuhi katika mji mkuu wa Baghdad, katika harakati ya kukabiliana na wanamgambo wa Kishia.Nalo bunge la Iraq limeitisha kikao cha dharura leo Ijumaa kujadilia njia za kumaliza ghasia zinazoendelea katika mji wa Basra.

Katika hatua nyingine Waziri mkuu Nuri al -Maliki amesema leo kuwa serikali yake itatoa pesa kwa wapiganaji ambao watasalimisha silaha zao hadi aprili 8,hatua ambayo inaweka mda mwingine mpya kwa wapiganaji wa Kishia, kusalimisha silaha zao.Mda wa kwanza alioutoa ulikuwa umalizike kesho jumamosi lakini tamko hili jipya linaonyesha kuwa mda umesogezwa mbele kwa kipindi cha wiki moja unusu.

Mbali na kusogezwa mbele kwa mda huo pia serikali yake imeahidi kutoa kitita cha fedha kwa wapiganaji hao ambao watasalimisha silaha zao.

Mwandishi wa habari wa shirika la habari la Reuters akiwa kusini mwa mji wa Nassiriya amesema kuwa wapiganajiwa wa kundi la Mahdi wamedhibiti eneo la kati la mji huo.Mji huo ni makao makuu ya mkoa wa Dhi Qar.

Amri ya kutotembea usiku imetangazwa katika mji wa Baghdad ili kukabiliana na ghasia,ambazo zimesabisha takriban watu 150 kupoteza maisha yao tangu serikali ilipoanzisha hujuma dhidi ya wafuasi wa Sadr siku ya jumanne ya wiki hii.

Mapema wiki hii kulitokea mapambano kati ya majeshi ya Marekani yakisaidia majeshi ya serikali dhidi ya wapiganaji wa mahdi.Eneo ambalo linalindwa sana mjini Baghdad la Green zone lilishambuliwa kwa mizinga.Mizinga hiyo ilikuwa inavurumishwa kutoka sehemu ambako wanapatikana washia wengi.

Msemaji wa jeshi la Marekani Kevin Berger hapo awali alisema kuwa licha ya kushambuliwa wao hawakurejesha mapigo kiholela kama walivyokuwa wakifanya wanamgambo wa kishia.

Lakini jeshi la Marekani katika taarifa lililoitowa leo ,linasema kuwa kikosi maalum cha waIraq ,SWAT, kikishirikiana na kikosi maalum cha Marekani kiliwauwa wanamgambo 14 na kuwajeruhi wengine 20 katika pambanao lililofanyika jumatano katika eneo la Kut.Wana kikosi cha ,SWAT, wapatao 9 waliuawa.

Pia taarifa za hivi punde kutoka Basra zinasema kuwa majeshi ya Iraq yamewauwa wanamgambo 120 kufikia sasa na pia kuwa majeshi ya ushirika yakiongozwa na Marekani, yameshambulia kwa mabomu, mitaa kadhaa ya mji wa Basra ambao ni ngome ya wapiganaji wa jeshi la Mahdi ambao ni watiifu kwa kingozi wa kidini wa kishia Moqtad al Sadr.