1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wito wa mkutano mkuu mpya wa Idadi ya watu duniani watolewa

21 Oktoba 2009

Baadhi wapendekeza 2014 au 20015

https://p.dw.com/p/KC3d

Pale mnamo wiki iliopita Umoja wa mataifa ulipoadhimisha miaka 15 tangu kufanyika mkutano wa kwanza kuhusu idadi ya wakaazi na maendeleo duniani 1994, moja wapo ya maswali yaliokuwemo katika fikra za wengi lilikua ni swali lililo wazi kabisa-nalo ni jee wakati umewadia wa kuandaa mkutano mkubwa kuhusu idadi ya wakaazi duniani ?

Umoja wa mataifa ambao umeandaa mikutano ya kimataifa kuhusu idadi ya watu duniani kila baada ya miaka 10 unazidi kukabiliwa na changamoto mpya za kiuchumi na kijamii kluhusiana na ongezeko la idadi ya watu, haki za uzazi, haki za jinsia na vitendo vya vitendo vya matumizi ya nguvu kama vile ubakaji.

Katibu mkuu wa umoja wa mataifa Ban Ki-Mooon anasema kwamba licha ya maendeleo ya kutia moyo yaliofanywa tangu ulipofanyika mkutano wa kimataifa kuhusu idadi ya watu na maendeleo duniani, bado kuna kiasi ya wanawake 200 milioni ambao wanashindwa kupata vidonge vya kuzuwia mimba vinavyofaa , wakati wanawake wengi mno hugeukia njia za utoaji mimba zisizo salama kwa sababu hawapatiwi elimu juu ya uzazi wa mpangilio.

Mkurugenzi mtendaji wa Shirika la idadi ya wakaazi duniani la umoja wa mataifa Thoraya Ahmed Obaid alisema hivi karibuni kwamba serikali 179 zilizoshiriki katika mkutano wa kimataiafa wa mjini Cairo kuhusu idadi ya watu na maendeleo miaka 15 iliopita, walichochea mabadiliko ambayo yanaendelea kuboresha maisha ya watu.

UN Frauenkommission UNFPA Thoraya Ahmed Obaid
Thoraya Ahmed Obaid,Mkurugenzi mtendaji wa Shirika la idadi ya watu duniani la Umoja wa mataifa (UNFP)Picha: UN Photo/Eskinder Debebe

Bibi Obaid alisema haki ya uazazi katika hali nzuri ya afya na kupewa usemi wanawake, ni nguzo kuu katika kulifungamanisha suala la idadi ya watu na maendeleo .

Alisema ajenda ya mkutano wa kimataifa wa Cairo inazingatia haja ya kuyashughulikia masuala ya haki za umma bila ya kujali hali zao, ikiwa ni pamoja na wahamiaji, wakimbizi na watu waliotawanyika, na kuifanya idadi ya watu, mazingira, amani na usalam pamoja na maendeleo kuwa mambo yenye kufungamana.

Akiulizwa juu ya kuendelezwa kwa mkutano wa kimataifa kuhusu idadi ya watu na maendeleo, mtazamaji wa kudumu katika umoja wa mataifa anayehusika na ushirikiano wa idadi ya watu na maendeleo, Jyoti Shnkar Singh,aliliambia shirika la habari la Reuters kwamba panahitajika maandalizi ya kina kabla ya kuwepo kwa mkutano mwengine wa dunia.

Akasema mkutano kama huo unahitaji kibali cha baraza kuu la umoja wa mataifa la wanachama 192 na utahitaji alau miaka miwili hadi mitatu ya maandalizi.Pamoja na hayo akaongeza kwamba kwa fikra zake mwaka 2014 au 2015 utakua wakati mwafaka kuwa na mkutano wa dunia.

Mkutano wa kwanza mkuu kuhusu iadadi ya watu duniani ulifanyika Romania 1974 ukifuatiwa na ule wa Mexico 1984 na 1994 ukafanyika nchini Misri.

Wito wa kuwa na mkutano mwengine mkuu kuhusu idadi ya watu duniani unakuja katika wakati ambao umoja wa mataifa unatoa kipa umbele katika suala la kufikiwa malengo yake ya manane ya milenia ifikapo 2015, ikiwa ni pamoja na kupunguza umasikini kwa 50 asili mia. Mengine ni kupunguza njaa, elimu ya msingi kwa wote, kushajiisha usawa wa jinsia, kupunguza idadi ya vifo vya watoto kwa theluthi mbili, vifo wakati wa kujifungua kwa robo tatu, kupambana na kutapakaa kwa virusi na ugonjwa wa Ukimwi, malaria na magonjwa mengine. Mengine ni kuhakikisha hifadhi ya mazingira na kukuza ushirikiano wa maendeleo kati ya nchi za kaskazini na kusini.

Mwandishi: Mohamed Abdul-Rahman /IPS

Mhariri:Abdul-Mtullya