1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wito wazidi kutolewa kuitaka Israel, kusimamisha mashambulio dhidi ya Gaza.

Halima Nyanza29 Desemba 2008

Wito wazidi kutolewa kuitaka Israel kusimamisha mashambulio yake dhidi ya Gaza, huku nchi hiyo ikipuuzia shutuma hizo zinazotolewa dhidi yake kutokana na kudai kuwa hatua hiyo ni kujilinda na mashambuo dhidi yake.

https://p.dw.com/p/GOoh
Mashambulizi yanayofanywa na Israel Ukanda wa Gaza, yamesababisha raia kadhaa wasio na hatia kuuawa, ikiwemo wanawake na watoto.Picha: AP

Mataifa na Jumuia mbalimbali za kimataifa zimeendelea kulaani mashambulio hayo yanayofanywa na Israel katika ukanda wa Gaza, kutokana na kuua raia wasio na hatia.

Uturuki na Misri zimeitaka Israel kusimamisha operesheni yake hiyo ya kijeshi huko Gaza, ambapo Waziri wa Mambo ya nchi za Nje wa Uturuki Ali Babacan akisema kuwa mashambulio hayo yatazidisha tu ghasia katika eneo hilo.

Naye Waziri wa Mambo ya chi za Nje wa Misri amesema nchi yake inalaani hatua hizo za kijeshi zinazochukuliwa na Israel kwa siku tatu mfululizo na kuongeza kuwa hali katika eneo hilo kwa sasa ni ya hatari.

Wakati Waziri wa Mambo ya nje wa Misri akisema hayo nchini mwake, maelfu ya watu wameandamana kupinga mashambulio hayo na kuitaka nchi hiyo kuchukua hatua dhidi ya Israel.

Waandamanaji hao pia wameilaumu serikali ya Misri kuufunga mpaka wake na Gaza.

Nchini Ujerumani, Kansela Angela Merkel ameshutumu Hamas kwa kuendeleza ghasia katika eneo hilo la mashariki ya kati, lakini pia ametoa wito kwa Israel, kuepuka kuua raia.

Msemaji wa Kansela wa Ujerumani Thomas Steg amesema, Bibi Merkel alifanya mazungumzo kwa njia ya simu na Waziri Mkuu wa Israel Ehud Olmert na kukubaliana kuwa Hamas inawajibika na hali hiyo kutokana na kuvunja makubaliano ya kusimamisha vita.

Serikali ya Afrika kusini nayo imeonya kuwa hali ni mbaya katika eneo hilo na kwamba ghasia hizo zinaweza kuenea katika maeneo ya jirani.

Naibu Waziri wa Mambo ya nchi za Nje wa Afrika kusini Fatima Hajaig amesema nchi yake imemuita balozi wa Israel Dov Segev Steinberg, kumuelezea kupinga kwao mashambulio yanayofanywa na nchi yake katika eneo la Gaza.

Katika hatua nyingine, kiongozi wa Hamas anayeishi uhamishoni Khaleda Meshaal yuko tayari kusaini makubaliano ya kusimamisha mapigano iwapo Israel itakubali kusimamisha mapigano na kuondoa vizuizi ilivyowekea Gaza.

Kiongozi huyo wa Hamas anayeishi uhamishoni ameyasema hayo wakati alipozungumza kwa njia ya simu na Rais Abdoullaye Wade wa Senegal, ambaye kwa sasa ndiye Mwenyekiti wa Jumuia ya nchi za Kiislamu OIC.

Katika hatua ya kulipiza kisasi, siku ya Jumamosi baada ya Shambulio la nguvu lililofanywa na Israel dhidi ya Gaza kiongozi huyo wa Hamas, Khaled Meshaal alitoa wito wa kufanya tena Intifada, uasi dhidi ya Israel, ikiwemo mashambulio ya kujitoa mhanga.

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia wakimbizi wa Kipalestina limearifu kuwa raia 57, 21 kati yao wakiwa watoto ni miongoni mwa watu 318 waliouawa mpaka sasa, ikiwa ni siku ya tatu mfululizo, tangu Israel ilipofanya shambulio la nguvu la anga dhidi ya Ukanda wa Gaza kwa lengo la kupambana na wapiganaji wa Hamas.

Aidha Wapalestina wenyewe wameitaka Jumuia ya Kimataifa kuingilia kati, kuweza kunusuru raia wasio na hatia wanaouawa katika mashambulio hayo.

Akijibu shutuma zinazotolewa dhidi ya nchi yake, Waziri wa Mambo ya nchi za nje wa Israel Tzipi(Tzipe Livne) Livni amesema nchi yake haina njia mbadala zaidi ya kushambulia Gaza.

Amesema nchi yake tayari imefanya kila iwezavyo, kuepukana na mashambulio hayo, lakini nchi yake haitaacha ishambuliwe na Hamas, kwani Israel imekuwa ikijaribu kukwepa kuua raia, wakati Hamas ikilenga kuua watoto wa nchi hiyo.

Israel inaendelea kusogeza vikosi vyake karibu na mpaka wa Gaza, tayari kwa mashambulio zaidi