1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wolfsburg na Hertha Berlin zatamba Bundesliga

9 Desemba 2013

Wolfsburg imesonga hadi nafasi ya tano baada ya kuinyamazisha Freiburg kwa kuifunga magoli 3-0, wakati nao Hertha Berlin ikiwachabanga Eintracht Braunschweig mabao 2-0 na kusonga katika nafasi ya saba.

https://p.dw.com/p/1AVXh
Picha: picture-alliance/dpa

Siku ya Jumamosi, Bayern walipata ushindi mkubwa wa mabao saba kwa sifuri dhidi ya Werder Bremen, ambao ulimfanya Pep Guardiola kukiri kuwa ilikuwa heshima kwake kuwa mwalimu wa Bayern wakati walipoirefusha rekodi yao ya kutoshindwa michuano 40 mfululizo katika Bundesliga. Hayo yalijiri wakati masaibu ya Borussia Dortmund yakiendelea kutokana na majeraha kikosini. Bayern iliikatakata safi ya ulinzi ya Bremen na kuiwacha ikiwa kama matambara, huku Franck Ribery akiwa moto wa kuotea mbali.

Nao Bayer Leverkusen wakapata ushindi muhimu wa goli moja kwa sifuri dhidi ya wenyeji Borussia Dortmund, ambao uliwawezesha kuwaruka vijana hao wa njano hadi nafasi ya pili wakiwa na tofauti ya pointi nne nyuma ya viongozi Bayern.

Awali, Borussia Moenchengladbach uilisonga katika nafasi ya nne ya msimamo wa ligi baada ya kuwalaza Schalke magoli mawili kwa moja. Kwingineko, Stuttgart iliwazaba Hannover mabao manne kwa mawili, Augsburg ikashinda goli moja kwa sifuri dhidi ya Hamburg, nao Hoffenheim wakashinda mbili moja dhidi ya Eintracht Frankfurt.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA

Mhariri:Mohammed Abdul-Rahman