1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Yaliyoandikwa magazetini hii leo

Hamidou, Oumilkher28 Februari 2008

Hukmu ya korti kuu ya katiba na BMW kupunguza idadi ya watumishi wake

https://p.dw.com/p/DF5k
Korti kuu ya katiba mjini KarlsruhePicha: AP



Uamuzi wa korti kuu ya katiba kuhusu kusachiwa mtandao na zana nyenginezo za mawasiliano ya kimambo leo,warsha ya mjini Bonn kwa vyama vinavyounda serikali kuu ya muungano mjini Berlin na mipango ya kampuni la magari la BMW kutaka kupunguza maelfu ya wafanyakazi ni miongoni mwa mada zilizochambuliwa na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo.


Kuhusu hukmu ya korti kuu ya katiba mjini Karlsruhe,gazeti la Die NEUE OSNABRÜCKER ZEITUNG linasema:


"Ni hukmu ya kihistoria,kwasababu mahakimu wamefanikiwa kubuni utaratibu wa aina yake wa kisheria.Wameunganisha masilahi ambayo kawaida si rahisi kuyaleta pamoja.Kwa upande mmoja mahakimu wanaweka vizingiti vya juu linapohusika suala la kuingiliwa watu katika mambo yao ya kibinafsi-kwa kile kijulikanacho kama "haki za kimsingi za Komputa".Mahakimu wanasema- "hadhi ya binaadam na uhuru wa kujiendeleza,inahusu pia mtambo wa Komputa mtu anaoumiliki".Kwa namna hiyo hukmu hiyo imepindukia vipimo vyote vilivyokuwepo.Kwa upande wa pili walinzi wa katiba wamezingatia hofu za idara za usalama,mitambo ya komputa isachiwe panapokua na uhakika timamu kuhusu mawasiliano ya watuhumiwa wa kigaidi .


Gazeti la SÜDDEUTSCHE ZEITUNG linahisi:


Korti kuu ya katiba imetambua umuhimu wa kuwepo kinga ya wanamtamdao.Umuhimu wa mtambo wa Komputor,kama sekta ya kibinafsi,unapindukia ule wa simu,nyumba au hata chumba cha kulalia.Amri ya kusachiwa mtambo huo inabidi isalie kua ya dharura.La sivyo wananchi watashindwa kuvumilia mlolongo wa sheria zinazohusiana na usalama.Athari zinazoweza kutokana na mpango wa kusachiwa komputa za watu zitakua kubwa mno kushinda faida za kuwasaka wahalifu.Kwa maneno mengine serikali inabidi iwe na tahadhari.Hukmu ya mahakama kuu ya katiba si idhini,ni onyo.


Gazeti la WESTDEUTSCHE ZEITUNG la mjini Düsseldorf linakwenda mbali zaidi na kuandika:


"Ni onyo hilo hasa kwa waziri wa mambo ya ndani Wolfgang Schäuble.Anaota ndoto ya uchunguzi mkubwa kupita kiasi.Pakiandikwa neno marufuku tuu katika Komputa ya mtu,maafisa wa idara ya upelelezi wanaingia mbioni na polisi wanamuandama mtuhumiwa gaidi na kumkamata akiwa bado juu ya meza ya Komputa.Yote hayo hayaambatani na katiba na ndio maana wanasheria wa mjini Karlsruhe wanazuwia."


Gazeti la SCHWERINER VOLKSZEITUNG limeandika kuhusu warsha ya vyama vinavyounda serikali kuu ya muungano mjini Berlin.Gazeti linaandika:


"Washirika wamemlani shetani .Wameonyesha wanaweza kuafikiana.Katika warsha yao huko Saintpetersberg karibu na Bonn wamebainisha wamechaguliwa ili kutawala na sio kushindana.Washirika katika serikali kuu ya muungano wamekubaliana kutia njiani mageuzi ya sera za kuwatunza wagonjwa,kuongezwa kiwango cha fedha za malipo ya nyumba kwa wasiojimudu na uwezekano wa kutumiwa nyumba mtu anayoimiliki kama sehemu ya malipo ya uzeeni.



Der SCHWARZWÄLDER BOTE lina maoni mengine kabisa:


"Ukiangalia kwa makini hutakosa kugundua vipengee tofauti vilivyomo ndani ya makubaliano hayo pamoja pia na kuyanyamazia masuala mengineyo.



Hatimae gazeti la FRANKFURTER ALLGEMEINE linazungumzia juu ya mpango wa kampuni la magari la BMW la kupunguza idadi ya wafanyakazi wake.Gazeti linaandika:


BMW halina shida yoyote.Mpaka leo kampuni hilo kubwa linaongoza miongoni mwa makampuni yanayojikingia mabilioni ya faida.Ndio maana watu wanashindwa kuelewa kwanini BMW inataka kufunga mkaja.Labda kudhoofika sarafu ya dola ya Marekani,bei za juu za mali ghafi na vifaa vyenginevyo,mashindano ya kibiashara sokoni na hatua kali za ulinzi wa mazingira,ndiyo mambo yanayoifanya BMW kupata shida ya kuuza magari mengi na ndio maana linalazimika kupunguza matumizi.



►◄