1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchaguzi Belarus

12 Oktoba 2015

Uchaguzi wa rais nchini Belarus na uwezekano wa kuondoshewa nchi hiyo vikwazo vya Umoja wa Ulaya,mashambulio ya mwishoni mwa wiki mjini Ankara nchini Uturuki na mzozo wa wakimbizi ni miongoni mwa mada magazetini.

https://p.dw.com/p/1Gmbr
Rais Alexander Lukaschenko wa BelarusPicha: Reuters/V.Fedosenko

Tuanzie lakini njia panda inayoiunganisha Belarus na Umoja wa Ulaya.Gazeti la "Märkische Oderzeitung" linaandika:"Kwakua kabla ya uchaguzi Lukaschenko aliwaachia huru baadhi ya wafungwa wa kisiasa,kuna wanaoashiria kwamba safari hii pengine vikwazo vya kiuchumi vya Umoja wa Ulaya vitapunguzwa makali.Vikwazo vile vile ambavyo viongozi wa Umoja wa Ulaya walivipitisha ili kupinga mitindo ya kukandamizwa upande wa upinzani.Wawakilishi wa upande huo wa upinzani,wakitanguliwa na mshindi wa tuzo ya Nobel ya fasihi kwa mwaka huu wa 2015, Swetlana Alexijewitsch wanazitahadharisha nchi za magharibi zisije zikaanza kumuamini Lukaschenko."

Gazeti la "Nordbayerischer Kurier" linaandika jinsi Swetlana Alexijewitsch anavyomnukuu kwa dhihaka muimla wa zamani Stalin alipotamka:"Muhimu sio nani kapiga kura,bali nani anazihesabu.Mshindi huyo wa tuzo ya fasihi ya Nobel,mzaliwa wa Belarus hajidanganyi,anatambua hakuna nchini mwake,si mbele na wala si nyuma anaeweza kumng'owa madarakani Alexander Lukaschenko anaeitawala nchi hiyo tangu mwaka 1994."

Sera za Erdogan zinamgeukia

Mashambulio ya kigaidi yaliyoangamiza maisha ya zaidi ya watu 97 mjini Ankara-mji mkuu wa Uturuki,yanatishia kuzisha ufa katika jamii ya Uturuki ambayo tokea hapo imegawanyika.Nini cha kufanya kuepukana na kuzidi makali mfarakano katika wakati huu wa mzozo wa wakimbizi?Gazeti la "Braunschweiger Zeitung" linaandika:"Kilichosalia ni kutaraji tu kwamba wale wanaopigania usawa kwa wote watashinda na sio wale wanaochochea mfarakano.Hali hiyo ni kwa masilahi ya Umoja wa Ulaya na hasa ya Ujerumani hasa kwa kuzingatia mzozo wa wakimbizi.Sera zake Erdogan zimemponza kwasababu akitaraji kutumia hali ya vitisho kuweza kujipatia faida za kisiasa.Hata hivyo kwa kumtenga Erdogan kisiasa,haimaanishi kwamba hali itoboreka.Hilo litawezekana tu ikiwa watu wataendelea kuzungumza nae na kutafuta njia ya kushawishi maamuzi yake."

Mzozo wa wakimbizi unaaendelea kupandisha mori

Mada yetu ya mwisho magazetini inahusu mzozo wa wakimbizi na mjadala mkali uliozukla humu nchini,hata miongoni mwa vyama vinavyounda serikali kuu ya muungano mjini Berlin.Gazeti la "Neue Osnabrücker Zeitung" linaandika:"Sauti nyengine zinasikika kuhusiana na mzozo wa wakimbizi:katika ushirikiano wa aina pekee chama cha Social Democratic SPD na kile cha kihafidhina cha CSU vinaonyesha kupigania pawepo maridhiano.Katika risala iliyoandikwa hivi karibuni na mwenyekiti wa SPD Sigmar Gabriel na waziri wa mambo ya nchi za nje Frank-Walter Steinmeier ,viongozi hao wawili wanasisitiza hofu za wananchi zizingatiwe-wanasema takriban yale yale yanayosemwa na CSU.Si ajabu:Hatari zaidi ingekuwa kulififiisha tatizo hilo na kuwaachia uwanja wafuasi wa siasa kali.Dhahir pia ni kwamba hoja kwamba hakuna kodi ziada za mapato ,wala ushuru utakaohitajika haziingiii akilini.Lakini kansela angezungumzia kinyume chake,ingebainisha kishindo halisi kilichoko."

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/INlandspresse

Mhariri:Yusuf Saumu