1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ziara ya Steinmeier Irak ishara ya nia njema

U.Leidholdt - (P.Martin)18 Februari 2009

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier anafanya ziara ya siku mbili nchini Irak.Lengo la ziara hiyo hasa ni kutoa ishara ya kisiasa kwa serikali mpya nchini Marekani.

https://p.dw.com/p/GwwQ
In this photo released by the Iraqi Government, Iraqi Prime Minister Nouri al-Maliki, right, meets Frank-Walter Steinmeier, the German foreign minister in Baghdad, Iraq, Tuesday, Feb. 17, 2009. (AP Photo/Iraqi Government) ** EDITORIAL USE ONLY **
Waziri wa Nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier(kushoto) akikutana na Waziri Mkuu wa Irak,Nouri al-Maliki(kulia)Picha: AP

Kwa ziara hii Steinmeier-aliekuwepo katika serikali ya kansela wa zamani Schroeder aliepinga uvamizi wa Irak - anataka kutoa ishara kuwa Ujerumani inarekebisha uhusiano wake na Washington.Kwani Ujerumani ilikataa kushiriki katika operesheni ya kijeshi ya George W.Bush iliyokwenda kinyume na sheria ya kimataifa.Operesheni hiyo imesababisha vifo vya Wairaki 180,000.Miaka sita baadae,Ujerumani ipo tayari kusaidia kuijenga upya nchi iliyoteketezwa na Saddam,vikwazo,vita na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe.

Ziara ya Steinmeier iliyopangwa tangu muda mrefu na kutangazwa baada ya Barack Obama kuchaguliwa rais wa Marekani imefanywa hivi sasa.Hii lakini si ziara ya kawaida kwani tarehe yenyewe iliwekwa siri mpaka dakika ya mwisho kwa sababu za usalama.

Mito ya Waziri Mkuu wa Irak Nouri al-Maliki kutaka msaada wa mashirika ya Kijerumani kuijenga upya nchi yake ambayo kwa sehemu kubwa haina umeme wala maji si jambo jipya.Hadi hivi sasa,mito hiyo haikuitikiwa.Irak bado ni eneo hatari ambako ni vigumu kwa mashirika ya kigeni kutekeleza kazi zake.Lakini al-Maliki kwa furaha anasema,hakuna tena ripoti za utekaji nyara katika televisheni.Kwa maneno mengine kisichoonekana,ndio hakipo pia. Ni wazi,ikiwa stesheni za televisheni nchini humo,kama ilivyokuwa Ijumaa iliyopita,hupigwa marufuku kuonyesha picha za mashambulio yaliyosababisha vifo vya waumini 40.

Ni kweli kuwa hali ya usalama imekuwa bora ikilinganishwa na hapo awali lakini hakuna siku inayopita bila ya machafuko kutokea:ikiwa ni vifo vinavyosababishwa na mabomu yanayozikwa kando ya barabara; mauaji yanayoamriwa;mashambulio ya kujitolea muhanga au mashambulio yanayochochewa kidini.Ni vizuri kwamba Ujerumani haikupeleka majeshi nchini Irak.Ni sahihi kwamba inashiriki katika miradi ya kukarabati sekta za elimu na afya panapowezekana.

Steinmeir asiiangalie ziara yake hiyo kuwa zaidi ya vile ilivyo-yaani ziara ya nia njema kwa rafiki mpya Mmarekani, atakaeondosha vikosi vyake huko Irak na kuvipeleka Afghanistan.Kushiriki katika jitahada za kiraia ni sawa, lakini iwapo Ujerumani kwa kufanya hivyo itaweza kujiepusha na mito ya Obama kushiriki zaidi kijeshi nchini Afghanistan ni suala jingine.