1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tsvangirai atoa masharti

Liongo, Aboubakary Jumaa25 Juni 2008

Kiongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini humo cha MDC,Morgan Tsvagirai aliyekimbilia katika ubalozi wa Uholanzi mjini Harare ametoa sharti la kuachiwa kwa Katibu wa chama chake, Tendai Biti, kabla ya kuwa na mazungumz

https://p.dw.com/p/EQqD
Kiongozi wa MDC Morgan Tsvangirai,akizungumza na waandishi wa habari nje ya ubalozi wa Uholanzi mjini HararePicha: AP

Tsvangirai alisema hayo katika mkutano na waandishi habari, kabla ya kurejea tena katika ubalozi huo alikokimbilia  toka siku ya Jumapili kwa kile alichosema kuokoa maisha yake.

Tsvangirai alisema kuwa hawezi kushiriki katika mazungumzo yoyote ya kuumaliza mzozo wa kisiasa nchi humo, mpaka atakapoachiliwa Tendai Biti pamoja na wafuasi wa chama hicho.


Tendai Biti alikamatwa mnamo wiki mbili zilizopita akituhumiwa na serikali ya Zimbabwe kwa makosa ya uhaini ambapo adhabu yake ni kunyongwa.


Aidha ameutaka Umoja wa Mataifa kupeleka majeshi ya kulinda amani nchini humo kwani Rais Mugabe ametangaza vita.


Wito huo pia umeungwa mkono na Waziri Mkuu wa Kenya Raila Odinga ambaye ameonya kuwa kama dunia haitochukua hatua stahiki itashuhudia kama yale yaliyotokea Rwanda mnamo mwaka 1994 ambapo zaidi ya watu laki nane waliuawa.


Kwa upande mwengine mbinyo dhidi ya utawala wa Mugabe kutaka kuahirishwa kwa duru ya pili ya uchaguzi wa urais, unazidi kuongezeka, ambapo Ufaransa imetangaza kuwa haitoutambua uchaguzi huo.


Msemaji wa Wizara ya Nje ya Ufaransa Pscale Andreane amesema kuwa nchi hiyo haitambua uhalali wa serikali itakayotokana na uchaguzi huo uliyopangwa kufanyika keshokutwa Ijumaa.


Mjini Mbabane, wakuu wa nchi wanachama wa kamati ya Ulinzi  na Usalama ya SADC wamekuwa wakikutana kujadili hali hiyo ya Zimbabwe.


Wakuu hao ni pamoja na Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania ambaye pia ni mwenyekiti wa Umoja wa Afrika,Eduardo do Santos wa Angola na Mfalme Mswati wa tatu wa Swaziland.


Rais Thabo Mbeki amesema kuwa hakualiakwa ingawaje Tanzania ilisema kuwa alialikwa.Mbeki ambaye ni mpatanishi wa nchi za SADC katika mzozo huo wa Zimbabwe amekuwa akilaumiwa kwa kuegemea upande wa Rais Mugabe.


Hata chama chake cha ANC ambacho kwa muda mrefu kimekuwa na uhusiano wa kidugu na chama cha Rais Mugabe cha ZANU PF kimetangaza wazi kutofurahishwa na utawala wa Mugabe.


Mjini London, Waziri Mkuu wa Uingereza Gordon Brown amesema kuwa nchi hiyo inajiandaa kwa vikwazo vikali zaidi dhidi ya utawala wa Harare.


Kwa upande mwengine mawaziri wa maendeleo kutoka nchi kumi zikiwemo Japan,Uingereza, Marekani, Ufaransa na Uswis wametoa taarifa wakizitaka nchi za SADC kuzidisha mbinyo kwa Rais Mugabe.


Mjini Harare, duru ya pili ya uchaguzi  wa urais, uliyopangwa kufanyika keshokutwa Ijumaa, imepata pigo lingine baada ya waangalizi huru wa ndani kutangaza kutoshiriki katika zoezi hilo.


Tume ya Uchaguzi ya Zimbabwe imeelezea kusikitishwa kwake na hatua hiyo ambayo inausogeza uchaguzi huo katika ncha ya kuwa batili.