1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Adidas yazindua Krasava

Bruce Amani
11 Novemba 2016

Kampuni ya Adidas imezindua mpira wa Krasava ambao utatumiwa katika michuano ya Kombe la Mashirikisho mwaka wa 2017. Mpira huo mweupe una mchoro wa mistari nyekundu ishara ya johari au mawe ya thamani ya Kirusi

https://p.dw.com/p/2SYun
Adidas Krasava Ball
Picha: adidas.com

Jina lake, Krasava, linaeleza neno linalotumiwa na mashabiki wa michezo wa Kirusi kusifia mchezo wa kusisimua.

Mpira huo utatumiwa kwa mara ya kwanza Novemba 14 kwenye mchuano wa kirafiki kati ya wenyeji wa dimba la Kombe la Mashirikisho na Kombe la Dunia 2018 Urusi na Romania. Kombe la Mashirikisho litachezwa katika miji minne ya Urusi kati ya Juni 17 na Julai 2, 2017.

Huwaleta pamoja mabingwa wa mashirikisho sita wanachama wa FIFA, pamoja na mabingwa wa dunia Ujerumani na wenyeji Urusi. Ureno (Ulaya), Australia (Asia), Mexico (Amerika ya Kaskazini, ya kati na Karibean), Chile ( Amerika Kusini) na New Zealand (Oceania) zimefuzu, wakati bingwa wa Afrika anasubiriwa.

Adidas ni mfadhili wa muda mrefu wa FIFA na pia ilitengeneza mipira iliyotumika katika mashindano yaliyopita ya Mashirikisho, kama vile Cafusa (Brazil 2013, Kopanya (Afrika Kusini 2009) na Pelias (Ujerumani 2005).

Mwandishi: Bruce Amani

Mhariri: Yusuf Saumu