1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Adly Mansour ndiye kiongozi mpya wa Misri

Admin.WagnerD4 Julai 2013

Jaji mkuu wa mahakama ya katiba nchini Misri ameapishwa kama rais wa muda baada ya jeshi kumng'oa madarakani Rais Mohammed Mursi huku kiongozi mkuu wa udugu wa kiislamu akikamatwa baada ya agizo la mwendesha mashitaka

https://p.dw.com/p/192Jx
Picha: Reuters

Adly Mansour ameapishwa leo katika mahakama ya katiba katika sherehe zilizoonyeshwa moja kwa moja kupitia televisheni ya kitaifa na kulingana na mamlaka za kijeshi, atahudumu kama kiongozi wa muda wa Misri hadi rais mpya atakapochaguliwa.

Katika hotuba yake ya kwanza Mansour ameyasifu maandamano yaliyosababisha kung'olewa madarakani kwa Mursi na kuwasifu vijana walioshiriki katika maandamano hayo yaliyoanza tarehe 30 mwezi uliopita.

Mansour amechukua mahala pa Mursi aliyeng'olewa madarakani hapo jana na jeshi baada ya mwaka mmoja uliogubikwa na misukosuko chungu nzima madarakani. Kwa sasa Mursi yuko chini ya kifungo cha nyumbani mahali kusikojulikana.

Rais wa muda wa Misri Adly Mansour
Rais wa muda wa Misri Adly MansourPicha: picture-alliance/AP

Viongozi wa kiislamu wasakwa

Mwendesha mashitaka nchini Misri leo alitoa agizo la kukamatwa kwa kiongozi wa chama cha Udugu wa Kiislamu, Mohammed Badie, na makamu wake, Khairat el Shater, na kupanua msako dhidi ya vuguvugu hilo, Hata hivyo katika hotuba yake ya kwanza, Mansour ametoa fursa kwa viongozi hao wa kiislamu kushirikishwa katika kile alichokiita ujenzi wa taifa na kuongeza kuwa hakuna atakayeachwa nje ya juhudi za kuijenga Misri iwapo watakubali wito huo.

Hali ya utulivu imerejea mjini Cairo leo baada ya umati mkubwa wa waandamanaji kukita kambi kwa siku tano hadi hapo jana na kusherehekea usiku kucha baada ya tangazo la jeshi la kupinduliwa kwa serikali ya Mursi.

Umoja wa Mataifa, Marekani na nchi nyingine zenye nguvu duniani hazikulaani kuondoelwa kwa Mursi kama mapinduzi ya kijeshi. Rais wa Marekani, Barack Obama, ambaye nchi yake inatoa msaada wa dola bilioni 1.3 kila mwaka kwa jeshi la Misri, ameelezea wasiwasi wake kwa kuondolewa kwa Mursi na kutaka kurejea haraka iwezekanvyo kwa serikali ya kidemokrasia iliyochaguliwa na wananchi.

Waandamanaji washerehekea baada ya kung'olewa madarakani kwa Mursi nchini Misri
Waandamanaji washerehekea baada ya kung'olewa madarakani kwa Mursi nchini MisriPicha: Reuters

Umoja wa Ulaya pia umetaka mchakato wa kidemokrasia kutekelezwa haraka iwezekanavyo. Mkuu wa sera za kigeni wa umoja huo, Catherine Ashton, amesema hilo lina maana kuwa kufanywe chaguzi za urais na bunge zitakazokuwa huru na haki na kuidhinishwa kwa katiba.

Nchi mbali mbali zazungumzia mapinduzi Misri

Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani, Guido Westerwelle, amesema hatua ya jeshi ni kurejesha nyuma hatua zilizopigwa za kidemokrasia na kutaka kuwe na majadiliano.

Chama cha rais wa Tunisia, Moncef Marzouki, kimelaani mapinduzi hayo ya kijeshi na kusema ni pigo kwa demokrasia na kwamba ni jaribio la kurejesha utawala wa zamani.

Maafisa wa idara ya mahakama nchini Misri leo wameanzisha uchunguzi dhidi Mursi na viongozi wengine 15 wa kiislamu kwa madai kuwa waliidunisha mahakama. Jaji Tharwat Hammad ametangaza marufuku ya kusafiri kwa wote hao. Hili ni agizo la pili la kumzuia Mursi kusafiri tangu jana.

Mwandishi: Caro Robi/afp/reuters/ap

Mhariri: Josephat Charo