1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrobarometer: Afrika ina ufahamu mdogo kuhusu tabianchi

Iddi Ssessanga
20 Agosti 2019

Licha ya kwamba Afrika ndiyo inaathirika zaidi mikondo isiyotabirika ya hali ya hewa duniani, utafiti mpya wa taasisi ya Afrobarometer umebainisha kuwa watu wengi barani humo hawaelewi kuhusu mabadiliko ya tabianchi.

https://p.dw.com/p/3OB0A
Südafrika
Picha: picture-alliance/AP Photo/N. Manie

Uharibifu mkubwa uliosababishwa hivi karibuni na kimbunga Idai kilichozishambulia nchi za kusini mwa Afrika za Msumbiji, Zimbabwe na Malawi, ni ukubusho usiofurahisha kwamba Afrika inabakia kuwa bara lililoko hatarini kwa kadri suala la kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi linavyohusika.

Utafiti mpya uliotolewa na Afrobarometer unachora taswira isiyo ya matumaini juu ya namna mazingira ya kilimo yanazidi kuwa mabaya kutokana na mvua zilizokawia, ubora wa maisha unaopungua na kinachoshangaza zaidi ya yote, maarifa kidogo au kutokuwepo kabisaa kwa ufahamu kuhusu madhara ya mabaliko ya tabianchi.

Utafiti huo umegundua kuwa kati ya mataifa 34 ya Afrika yaliofanyiwa utafiti, washiriki katika mataifa 30 walisema uzalishaji wa kilimo umepungua kwa kiasi kikubwa kutokana na ukame katika kipindi cha muongo uliyopita.

Food and Agriculture Organization of the United Nations bekämpfen Würmer
Afrisa wa shirika la chakula na kilimo duniani (FAO) akizungumza na wakulima.Picha: FAO

Mratibu wa mawasiliano wa Afrobarometer Gugu Nonjinge, aliiambia DW kuwa wakulima nchini Uganda wamekuwa wakisubiri mvua bila ukomo, na Afrika Kusini imeshuhudia mafuriko kupita kiasi.

Katika utafiti huo, ujuzi kuhusu mabadiliko ya tabianchi ulielezwa kama kutambua kwamba mshiriki anajua kuhusu mabadiliko ya tabianchi, anaiyahusisha na mabadiliko hasi ya hali ya hewa na anatambua kwamba shughuli za kibidamu zinatoa mchango mkubwa katika mabadiliko ya tabianchi kutokana na utoaji wa gesi chafu ya ukaa.

Wakati asilimia 58 ya Waafrika walisema wamesikia kuhusu mabadiliko ya tabianchi, wanne katika kila kumi walikiri kwamba hawakuwahi kusikia kuhusu neno hilo kabla.

Nonjinge alisema Abfrobarometer iliwatambua wale wanaofanyakazi kwenye sekta ya kilimo katika maeneo ya vijijini, maskini, wanawake na wenye kiwango duni cha elimu, kama wasio na ufahamu kuhusu mabadiliko ya tabianchi.

Maarifa juu ya mabadiliko ya tabianchi

Elfenbeinküste Bananenplantage
Afrika ndiyo inaathirika zaidi na mabadiliko ya tabianchi, lakini wengi wa wakaaziwake hawana ufahamu juu ya suala hilo.Picha: Getty Images/AFP/I. Sanogo

Wengi waliojua na kuelewa maana ya mabadiliko ya tabianchi walisema kubalikabadilika kwa hali ya hewa kumeyafanya maisha kuwa mabaya zaidi katika mataifa yao. Bara la Afrika ndiyo liko kwenye hatari kubwa zaidi kukumbwa na madhara ya mabadiliko ya tabianchi.

Cha kushangaza lakini, utafiti huo ulibaini kuwa masuala muhimu kama vile uhaba wa maji, usalama wa chakula na kilimo, vilivyotajwa na wale waliohojiwa vinahusiana moja kwa moja na mabadiliko ya tabianchi.

Afrika imetia saini mikataba kadhaa ya kimataifa kama vile wa Kyoto na makubaliano ya Paris ya 2015 kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi. Makubaliano haya ya kimataifa yanalenga kupambana na kurudisha nyuma athari za mabadiliko ya tabianchi.

Utafiti wa Afrobarometer unapendekeza kwa serikali za Afrika, watunga sera na wanaharakati kuboresha uelewa juu ya mabdiliko ya tabianchi ili kujenga jamii yenye maarifa inayoelewa vitisho vya mabadiliko ya tabianchi na itakayosaidia juhudi za pamoja za serikali na kimataifa.

Chanzo: Afrobarometer