1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Burundi matatatani

15 Mei 2015

Wiki hii magazeti ya Ujerumani yanatoa maoni juu ya hali ya kisiasa nchini Burundi. Na pia yameandika juu ya mabadiliko yaliyofanyika katika uongozi wa chama cha upinzani nchini Afrika Kusini ,Demoratic Alliance.

https://p.dw.com/p/1FQS8
Waziri wa maendeleo wa Ujerumani Gerd Müller
Waziri wa maendeleo wa Ujerumani Gerd MüllerPicha: AFP/Getty Images/R. Hartmann

Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" limechapisha makala juu ya Waziri wa maendeleo wa Ujerumani, Gerd Müller anaehubiri juu ya harakati za kupambana na umasikini na njaa.

Gazeti la "die tageszeitung" linasema hata kama jaribio la kuiangusha serikali lingefanikiwa nchini Burundi,hakuna anaejua iwapo hiyo ingelikuwa njia sahihi.

Gazeti la "die tageszeitung linasema ni jambo la kulitilia maanani sana kwamba watu katika mji mkuu wa Burundi walijitokeza kwa wingi barabarani kumpinga Rais anaewania muhula wa watu kinyume na katiba.

Gazeti la "die tageszeitung" linasema jambo la kulitilia maanani zaidi ni kwamba watu hao waliziweka kando taofauti za kikabila na milengo yao ya kisiasa ili kusimama pamoja na kumpinga Rais wao. Na ndiyo sababu, gazeti hilo linahoji kwamba jaribio la kumwondoa Rais Nkurunziza madarakani linapaswa kuzingatiwa kama hatua ya kumwonyesha Rais huyo mipaka ya mamlaka yake na lisiangaliwe kama jaribio la kutwaa mamlaka kwa nguvu za kijeshi!

Chama cha upinzani chaibadilisha rangi ya ngozi Afrika Kusini

Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" wiki hii linatupasha habari juu ya mabadiliko yaliyofanyika katika uongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini humo, Democratic Allliance. Hata hivyo mabadiliko hayo siyo ya sera ,bali ni ya rangi ya ngozi.

Gazeti hilo linaeleza kwamba chama cha kisiasa ambacho mpaka sasa kimekuwa kinatambulika kama cha wazungu tu,nchini Afrika Kusini, kimepata mwenyekiti mpya ambae ni mweusi Mmusi Maimane. Hata hivyo gazeti la "Frankfurter Allgemeine" limesema kwamba chama kinachotawala nchini Afrika Kusini,African National Congress kimeyabeza mabadiliko hayo.

Chama cha ANC kimesema Maimane ni mzawa wa kukodisha na kwamba yeye ni kama nazi, nje mweusi lakini ndani mweupe.

Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" linakumbusha kwamba aliekuwa Mwenyekiti wa chama hicho, mpaka sasa Hellen Zille ambae ni mzungu alikuwa anawaziwakilisha pande mbili za ukweli.

Kwanza amekiletea chama chake cha DA mafanikio. Katika uchaguzi wa bunge mwaka uliopita, chama hicho kilipata asilimia 22. Lakini jambo la pili, gazeti linasema , ni kwamba ilikuwa rahisi kwa chama kinachotawala ANC ,kusema kwamba chama hicho cha upinzani kilikuwa cha wazungu wachache wanaotaka kuurejesha utawala wa kibaguzi nchini Afrika Kusini.

Na juu ya mabadiliko yaliyofanywa katika uongozi wa chama cha Democratic Alliance gazeti la "Frankfurter Allgemeine" linasema iwapo kiongozi huyo mweusi, Maimane ambae ni mchungaji ataiinua hadhi ya chama chake nchini kote itaonekana hapo baadae.

Mhubiri wa harakati dhidi ya umasikini

Gazeti hilo pia limeandika juu ya Waziri wa maendleo wa Ujerumani Gerd Müller.Gazeti hilo linamwita Waziri huyo kuwa mtu mwenye uwezo mkubwa wa kuona mbali.

Gazeti hilo linasema Waziri Gerd Müller amefanikiwa. Amejenga umaarufu wake haraka kutokana na kuhubiri juu ya harakati za kupambana na njaa na umasikini. Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" linatilia maanani kwamba Waziri Müller anataka kuiokoa dunia.


Gazeti hilo limearifu kwamba baada ya kutokea maafa ya wakimbizi kwenye bahari ya Mediterania Waziri huyo wa Ujerumani anataka Euro Bilioni 10 zimegwe kutoka kwenye mfuko wa vitega uchumi wa Umoja wa Ulaya na zitumike kwa ajili ya kuyafanya maisha ya watu yawe bora katika nchi ambako wakimbizi wanatoka.Lakini gazeti la Frankfurter Allgemeine "limesema baadhi ya matatizo katika fulani za Afrika hayawezi kutauliwa kwa njia ya fedha peke yake.

Gazeti la " die tageszeitung linatuarifu kwamba Kiongozi wa kundi la kigaidi la ADF Jamil Mukulu kutoka Uganda amekamatwa nchini Tanzania. Kundi hilo la ADF limekuwa linawaua raia katika mji wa Beni mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.


Mwandishi: Mtullya Abdu

Mhariri: Josephat Charo