1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kilimo muhimu kwa ajira

11 Julai 2015

Wiki hii magazeti ya Ujerumani yameandika juu ya matokeo ya uchaguzi wa Bunge nchini Burundi na jinsi Wajerumani wanavyopaswa kuyakumbuka waliyoyafanya nchini Namibia wakati wa ukoloni

https://p.dw.com/p/1Fx3x
Waherero wasimama kidete dhidi ya wakoloni wa kijerumani
Waherero wasimama kidete dhidi ya wakoloni wa kijerumaniPicha: Bundesarchiv/183-R18799

Juu ya Burundi gazeti la "die tageszeitung linasema matokeo ya uchaguzi wa bunge uliofanyika nchini humo yanapaswa kuwa chapuo ya kuwahamasisha wapinzani .

Gazeti hilo pia limeyatilia maanani maazimio yaliyopitishwa na viongozi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwenye mkutano wao uliofanyika mjini Dar-Es-Salaam. Gazeti la "die tageszeitung" linasema viongozi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wanaimarisha shinikizo dhidi ya Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi anaewania kugombea muhula wa tatu wa urais .

Gazeti la "die tageszeitung " limeyatilia maanani mambo muhimu yaliyoamuliwa kwenye mkutano wa viongozi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.Kwanza kuitaka serikali ya Burundi iahirishe uchaguzi wa rais na pili Burundi ichukue hatua ya kuunda serikali ya umoja wa kitaifa.

Tawi la Imbonerakure livunjiliwe mbali

Gazeti la "die tageszeitung" pia limetilia maanani kwamba viongozi wa jumuiya ya Afrika Mashriki wanataka tawi la vijana,wanaoitwa Imbonerakure livunjiliwe mbali chini usimamizi wa Umoja wa Afrika.


Hata hivyo gazeti hilo limeikariri taarifa ya chama tawala nchini Burundi CNDD-FDD iliyosema kwamba chama hicho kimelisikia shauri hilo la kuahirisha uchaguzi wa rais lakini kimesema hatua hiyo ni jambo lisilowezekana.

Gazeti la "die tageszeitung" wiki hii pia limekumbusha juu ya enzi za ukoloni wa Wajerumani nchini Namibia, wakati unatimia mwaka wa mia moja tangu enzi hizo zifikie mwisho. Gazeti hilo limemnukuu msemaji wa masuala ya utamaduni wa chama cha kijani nchini Ujerumani Ulle Schaws akisema kwamba Ujerumani haiwezi kuifuta historia yake.

Gazeti la "die tageszeitung" limemkuklu msemaji huyo Schaws akiitaka Ujerumani iukubali wajibu wake wa kihistoria juu ya Namibia na hasa juu ya mauaji ya waherero.

Kilimo muhimu kwa ajira

Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" linasema sekta ya kilimo inaweza kutoa ajira kwa mamilioni ya watu katika nchi za Afrika, mradi tu kilimo hicho kiwe cha kisasa.

Gazeti hilo linakumbusha kwamba miaka miwili iliyopita, Benki ya Dunia ilitoa mwito kwa nchi za Afrika wa kuongeza uzalishaji katika kilimo ili sekta hiyo iwe injini ya ustawi barani Afrika. Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" linaeleza kwamba wakati huo nchi za Afrika zilikuwa zinaagiza bidhaa za chakula zenye thamani ya dola Bilioni 25 hasa kutoka nchi za Asia. Lakini hakuna alieataka kuitikia mwito wa Benki ya Dunia.

Sababu ni kwamba nchi za Afrika zimekuwa zinafikia ustawi wa zaidi ya asilimia 4 kwa mwaka kutokana na mauzo ya malighafi. Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" limemnukulu mwenyekiti wa shirika la maendeleo ya kilimo duniani,Kanayo Mwanze akisema kwamba nchi za Afrika zinaruzuku nafasi za ajira katika nchi za Asia.

Kanayo Mwanze anaetokea Nigeria alikaririwa na gazeti hilo akisema hayo baada ya kutambua kwamba gharama za kuagiza chakula kutoka Asia ziliongozeka kwa nchi za Afrika na kufikia dola Bilioni 38.

Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" limearifu kwamba Mwenyekiti huyo wa shirika la maendeleo ya kilimo duniani,sasa anafanya ziara katika nchi za Afrika kwa lengo la kuzihimiza nchi hizo ziweke mkazo katika kilimo ili kutenga nafasi za ajira na ili sekta hiyo iwe injini ya ustawi barani Afrika.

Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" linatilia maanani kwamba kuna unomi katika nchi nyingi za Afrika.Kenya, Msumbiji na Tanzania zinafikia ustawi wa zaidi ya asilimia 6 .mchango mkubwa unatolewa na mauzo ya maliasilia kama vile, mafuta na madini. Gazeti linasema wakati ustawi mkubwa unatokana na maliasilia barani Afrika, chakula kwa ajili ya watu wa bara hilo kinazalishwa kwingineko

Mwandishi:Mtullya Abdu/Deutsche Zeitungen.

Mhariri:Yusuf Saumu