1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika katika magazeti ya Ujerumani

Zainab Aziz
5 Januari 2018

Wiki hii magazeti ya Ujerumani yameandika juu ya tangazo la kuachiwa huru kwa wafungwa wa kisiasa nchini  Ethiopia, uhaba wa maji katika jiji la Cape Town na pia kuhusu wapinzani kugawanyika nchini Sudan Kusini.

https://p.dw.com/p/2qPdB
Äthiopien kündigt Freilassung politischer Gefangenen an | Hailemariam Desalegn
Desalegn
Picha: picture alliance/AA/E. Hamid

Süddeutsche Zeitung

Waziri  mkuu  Desalegn  amesema anakusudia kuupanuza wigo wa kidemokrasia kwa manufaa ya wananchi wote  wa  Ethiopia. Kwa kulitoa  tangazo hilo waziri mkuu huyo amekiri  kwamba wapo wafungwa  wa kisiasa  katika  jela  za nchi yake, hata hivyo idadi ya watu hao haijulikani. Kinachojulikana ni kwamba maalfu ya watu wamekamatwa tangu kuanza kufanyika maandamano ya kuipinga serikali mnamo mwaka wa 2015. Gazeti hilo la Süddeutsche pia linatilia maanani kwamba serikali ya Ethiopia  inakusudia  kuifunga jela ya kinyama ya Maekelawi, inayojulikana kwa kuwatesa wafungwa.

Gazeti hilo la Süddeutsche limewakariri wapinzani, wanaharakati na watetezi haki za binadamu wakisema kwamba wafungwa wa kisiasa kwenye  jela  hiyo wamekuwa wanateswa kwa miaka mingi kwa lengo  la kuwalazimisha wakubali makosa yao. Gazeti hilo pia linaeleza kwamba waziri mkuu wa Ethiopia anataka uchunguzi ufanyike  juu ya  kukiukwa haki za binadamu kwenye  jela hiyo.

Neues Deutschland

Gazeti la Neues Deutschland wiki hii linaripoti kwamba wapinzani wamegawanyika nchini Sudan Kusini. Limeandika kwamba hali hiyo imetokea baada ya kuvunjika kwa mkataba wa amani uliotiwa  saini mnamo  mwaka 2015  baina  ya rais  Salva Kiir  na hasimu wake ambaye pia aliwahi kuwa makamu wake, Riek Machar. Gazeti hilo linasema  vita nchini Sudan Kusini vimekithiri kwa ukatili na kusababisha maalfu kwa maalfu ya watu waikimbie nchi yao.

Kwa mujibu wa gazeti hilo la Neues Deutschland idadi ya watu wanaokimbia Sudan Kusini na kuingia Uganda imekuwa inaongezeka kila siku, wakimbizi kutoka Sudan Kusini wameshafikia zaidi ya milioni moja nchini Uganda. Wanapowasili nchini humo watu hao wanatoa taarifa jinsi wapiganaji wa kabila la Dinka la rais  Salva Kirr wanavyowaandama watu  wa makabila madogo. Gazeti hilo linafahamisha  zaidi.

Makundi ya waasi  nchini Sudan Kusini pia yamegawanyika katika msingi  wa makabila, ikiwa pamoja  na yale ya Wakaakwa na Wakuku kiasi kwamba wapiganaji wa kabila la Nuer la aliyekuwa makamu wa rais Riek Machar hasimu mkuu wa rais  Salvar Kiir sasa hawana tena ushawishi mkubwa  nchini Sudan  Kusini. Hofu imetanda nchini humo kutokana na mauaji.

Hata hivyo gazeti hilo la Neues Deutschland linasema  inashangaza kutambua kwamba Umoja wa Mataifa bado  haujaiona hali hiyo kuwa ni mauaji  ya halaiki. Vita vya hapo awali baina ya  wanasiasa wawili, Salvar Kiir na Riek Machar  sasa  vimegeuka kuwa vya makabila karibu yote ya Sudan Kusini.

Berliner Zeitung

Gazeti la Berliner Zeitung linatupeleka katika jiji la Cape Town linalojulikana kuwa lulu ya  utalii  nchini  Afrika  Kusini. Gazeti hilo linafahamisha kwamba ugavi wa maji umo katika hali ya dharura na linaeleza kwamba maji yamezidi kuwa haba katika jiji la Cape Town kiasi kwamba kumtakia mtu heri ya mwaka mpya ni sawa na kumdhihaki. Katika  siku ya kwanza ya mwaka  mpya wakaazi wa jiji hilo walipewa tahadhari nyingine wakitakiwa wabane zaidi matumizi ya maji.

Gazeti hilo la Berliner limesema ikiwa mvua haitanyesha katika kipindi  cha miezi minne ijayo mabomba yatakuwa  yanafoka hewa ya moto tu. Gazeti hilo linaeleza kuwa ikiwa hali itafikia hatua hiyo katika jiji la Cape Town,  hiyo itakuwa mara  ya kwanza katika historia ya miji kwa  binadamu  kukaukiwa  maji kabisa. Gazeti la Berliner linasema dharura inayotokana na uhaba wa maji  inatishia kuathiri miundo mbinu, kilimo na  afya za wakaazi wa jiji  la Cape Town.

Watu wapimiwa kiasi cha maji

Berliner Zeitung linafahamisha  kwamba  kuanzia  jumatatu  iliyopita, kila mtu anaruhusiwa lita 87 tu za maji kwa siku. Wakulima wanatakiwa  wapunguze matumizi kwa asilimia  45, pia ni marufuku kumwagilia maji bustani au kuosha magari. Miaka15 iliyopita, viongozi wa jiji  la Cape Town walitahadharishwa juu ya  hatari  ya jiji lao kukumbwa  na  ubaba wa  maji wa kiwango kikubwa  kutokana na kuongezeka  idadi  ya  wakaazi.

Katika kipindi cha miaka 25 iliyopita idadi  ya watu imeongezeka kutoka milioni mbili hadi kufikia zaidi ya watu milioni nne lakini ongezeko hilo la watu halikwenda sambamba na ongezeko la ugavi wa maji. Mbali na hayo jiji  la Cape Town  limekumbwa na ukame usiokuwa na kifani katika kipindi  cha miaka  miaka mia moja iliyopita. Kiasi cha dola milioni 210 kinahitajika kwa ajili ya kujenga mtambo wa kuchuja maji ya chumvi ya kutoka baharini ili kuweza  kukidhi mahitaji ya wakaazi  wote.

Mwandishi:Zainab Aziz/Deutsche Zeitungen

Mhariri:  Gakuba, Daniel