1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika katika magazeti ya Ujerumani

Zainab Aziz Mhariri: Josephat Charo
17 Mei 2019

Baadhi ya yale yaliyoandikwa kwenye magazeti ya Ujerumani juu ya Afrika wiki hii ni pamoja na matumaini ya kupatikana demokrasia nchini Sudan na malalamiko kuhusu mpango wa mafunzo wa jeshi la Ujerumani nchini Niger.

https://p.dw.com/p/3If4p
Afrika | Protests im Sudan
Picha: picture-alliance/dpa/AA/M. Hjaj

 die tageszeitung 

Yapo matumaini ya kupatikana demokrasia nchini Sudan lakini jeshi bado lina nguvu na raia wameachwa peke yao. Wanajeshi na viongozi wa harakati za upinzani wameshapatana juu ya baraza la kipindi cha mpito litakaloongoza nchi kwa muda wa miaka mitatu hadi uchaguzi utakapofanyika lakini hadi kufikia lengo hilo bado pana hatua. Jeshi bado lina mamlaka.

Wiki iliyopita watu waliokuwa wamevalia sare za jeshi ambao hawajatambulika waliwashambulia wanajeshi na waandamanaji mjini Khartoum. Gazeti la die tagesezutng linasema shambulio hilo ni ishara ya tahadhari kwa wanajeshi na wapinzani kwamba mabadiliko yoyote lazima kwanza yapitie mtihani na kwamba wako watu wenye uwezo wa kuyatetea maslahi yao kwa njia ya silaha.

Süddeutshce

Gazeti la Südeutsche limeandika juu ya malalamiko yaliyotolewa kuhusu mpango wa mafunzo yanayotolewa na wanajeshi wa Ujerumani kwa jeshi la Cameroon. Gazeti hilo linasema mpango huo ni makosa na ni wa hatari na linaeleza kwamba baada ya Ujerumani kukosolewa juu ya mpango wa kikosi chake maalumu cha jeshi, wa kutoa mafunzo kwa jeshi la Niger sasa Ujerumani imeingia katika lawama nyingine. Safari hii ni juu ya mpango  wa mafunzo yanayotolewa kwa jeshi la Kamerun.

Gazeti hilo limemnukulu msemaji wa masuala ya nje wa chama cha mrengo wa shoto akisema kuwa mpango huo ni makosa na ni wa hatari. Msemaji huyo ameeleza kwamba jeshi la Ujerumani linatoa mafunzo katika nchi iliyomo katika vita vya wenyewe kwa wenyewe. Gazeti hilo la Südeutsche linatilia maanani kwamba kama ilivyokuwa nchini Niger, wakufunzi wa jeshi la Ujerumani wako nchini Cameroon bila ya idhini ya bunge la Ujerumani.

Neue Zürcher

Gazeti la Neue Zürcher linatuarifu kwamba katika muda wa miezi 20 iliyopita watu 1850 waliuawa kutokana na mgogoro wa jimbo ???? nchini Cameroon, ambako lugha ya Kiingereza inatumika.

Neues Deutschland

Gazeti la Neues Deutschland linatupeleka katika jimbo la Puntland ambalo ni sehemu ya kaskazini mashariki ya Somalia, ililoyojitangazia mamlaka ya ndani mnamo mwaka 1998. Gazeti hilo linazungumzia juu ya mkasa wa kubakwa na kuuliwa kwa, Aisha, msichana aliyekuwa na umri wa miaka12. Gazeti hilo linasema kwamba mikasa ya ubakaji imetokea mara kwa mara katika jimbo la Puntland lakini hadi sasa imekuwa inazingatiwa kama makosa madogo tu.

Uhalifu huo unapuuzwa pia na Polisi na taasisi za kisheria. Hata hivyo mkasa wa marehemu Aisha, umetifua tufani katika Puntland. Wazazi wake walifanya kila waliloweza hadi ulishughulikiwa jinsi ilivyopasa. Mitandao ya kijamii na vyombo rasmi vya habari viliingilia kati na  kuujadili kwa nguvu zote. Mjadala uliwahamasisha watu walioandamana kudai haki itendeke. Watu watatu waliotenda uhalifu wa kumbaka na kumuua Aisha walifikishwa mahakamani na kuhukumiwa adhabu ya kifo. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza, kutumika kwa sheria iliyowekwa miaka mitatu iliyopita, ya kuwaadhibu  vikali watu wanaotenda uhalifu wa ubakaji.

Frankfurter Allgemeine

Gazeti la Frankfurter Allgemeine limendika makala juu ya historia ya Afrika ambayo imeibwa na wakoloni. Makala hiyo inatokana na mkutano uliofanyika juu ya ukoloni wa nchi za Ulaya barani Afrika. Gazeti hilo linaeleza kwamba Ulaya imeiba historia ya Afrika. Huo ni msimamo wa wataalamu wa Afrika, na siyo tu juu ya vitu kama vinyago vilivyoporwa na Wafaransa, Wajerumani na waingereza bali pia juu ya historia ya bara  hilo.

Mtaalamu wa historia Nwando Achebe kutoka Nigeria aliyehudhuria mkutano juu ya historia ya Afrika uliofanyika mjini Berlin mwanzoni mwa wiki hii amelalamika kuhusu athari kubwa ya wataalamu wa Ulaya juu ya historia ya Afrika. Achebe amesema siyo kwamba historia ya Afrika imeandikwa na watu wa Ulaya bali bado wanaendelea kuidhibiti historia hiyo mpaka leo. Gazeti  la Frankfurter Allgemeine limemnukulu profesa Achebe akisema kuwa nchi za Ulaya bado zinaendelea kung'ang'ania maslahi yao bila ya kujali maslahi ya waafrika.

 Vyanzo: Deutsche Zeitungen