1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika katika magazeti ya Ujerumani

Zainab Aziz Mhariri: Chilumba Rashid
22 Machi 2024

Yaliyoandikwa kwenye magazeti ya Ujerumani juu ya Afrika mnamo wiki hii ni pamoja na juhudi za kupambana na maambukizi ya virusi vya corona katika nchi za Afrika na juu ya uchaguzi wa rais uliofanyika nchini Gambia.

https://p.dw.com/p/445S3
Südafrika ein Covid Graffiti in Johannesburg
Picha: Jerome Delay/AP Photo/picture alliance

Frankfurter Allgemeine Zeitung

Gazeti la Frankfurter Allgemeine juu ya juhudi za kupambana na maambukizi ya virusi vya corona katika nchi za Afrika. Gazeti hilo linasema mpaka sasa Afrika imebaki nyuma katika mchakato wa kutoa chanjo dhidi ya corona. Gazeti hilo linatilia maanani kwamba wakati asilimia 43 ya watu kwingineko duniani wameshapatiwa chanjo, barani Afrika mpaka sasa ni asilimia 7 tu. Sababu ni  kwamba dawa hizo zilizotolewa kwa hisani bado hazijawafikia wahitaji.

Gazeti la Frankfurter Allgemeine linaeleza kwamba nchi tajiri zimetoa ahadi ya kuzifadhili  nchi za Afrika lakini dawa hazijafika zinakokusudiwa. Mpaka sasa nchi hizo tajiri zimeweza kupeleka thuluthi moja ya dozi ilizoahidi. Gazeti hilo linasema tatizo kubwa linatokana na mazungumzo juu ya mikataba kati ya wahisani na wahitaji.

Süddeutsche Zeitung

Gazeti la Süddeutsche limeandika juu ya virusi vya aina ya Omicron vilivyosabisha hatua ya kuziwekea nchi za Afrika vizuizi. Gazeti hilo llimemnukulu Rais Lazarus Chakwera wa Malawi akisema watu wote wana wasiwasi juu virusi hivyo na kwamba hatua  iliyochukuliwa na baadhi ya nchi za magharibi kuziwekea vizuizi vya safari nchi za kusini mwa Afrika siyo jambo la linalostahili. Rais huyo wa Malawi amesema dunia inapaswa kuwashukuru wanasayansi wa Afrika Kusini kwa kuving'amua virusi hivyo vya Omicron. Rais Chakwera amewataka watu wazingatie sayansi badala ya ubaguzi.

Gazeti la Süddeutsche limetoa mfano wa taarifa zlizoandikwa kwenye magazeti ya Ulaya. Kwa mfano gazeti moja la Ujerumani lilionyesha picha ya mama na mtoto wake na kusema virusi kutoka Afrika vimewasili kwetu Ujerumani. Hata hivyo gazeti hilo la Ujerumani linaloitwa Die Rheinfalz limeomba radhi. Gazeti la Süddeutsche limesema taarifa hiyo kwenye gazeti la Ujerumani zimewakasirisha watu kwenye nchi nyingi za Afrika. Linaeleza kwamba virusi vya Omicron vimeripotiwa kwa mara ya kwanza na wanasayansi wa Afrika Kusini lakini haina maana kwamba nchi hiyo ndiyo chimbuko la janga hilo! Süddeutsche linasema watu zaidi ya 250 wamepatikana na virusi hiyvo nchini Uingereza lakini nchi hiyo haijawekewa vizuizi na nchi nyingine.

Neue Zürcher

Gazeti la Neue Zürcher lianazungumzia juu ya uchaguzi wa rais uliofanyika nchini Gambia. Linasema uchaguzi huo ulikuwa mtihani mgumu kwa nchi iliyopo kwenye eneo ambapo serikali za nchi kadhaa zimeangushwa kwa njia ya mtutu wa bunduki. Gazeti la Neue Zürcher linasema watu wa Gambia wamemchagua tena rais aliyemo madarakani Adama Barrow aliyepata asilimia 53 ya kura.

Gazeti hilo linatilia maanani kwamba uchaguzi wa Gambia ulikuwa mtihani mgumu kwa demokrasia ya nchi hiyo. Kuanza mwaka 1994 hadi mwaka 2014 Gambia ilipitia wakati mgumu chini ya uongozi wa rais Yahya Jammeh. Gazeti la Neue Zürcher limemnukulu mshindi wa uchaguzi rais Adama Barrow akisema kuwa demokrasia imeshinda nchini Gambia,  linasema licha ya madai juu ya kutokea hitilafu, uchaguzi wa nchini Gambia umeleta  mwanga katika eneo la giza!

die tageszeitung

Nalo gazeti la die tageszeitung linazungumzia juu ya mashambulio yaliyofanywa na  wanajeshi wa Uganda dhidi ya waasi wenye itikadi kali. Waasi hao kutoka Uganda wa kundi la ADF wanalaumiwa kufanya mauaji mara kwa mara ndani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. die tageszeitung linaeleza kwamba watu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wamefurahi juu ya hatua iliyochukuliwa na wanajeshi wa Uganda.

Gazeti hilo limewanukulu wakaazi wa Kivu kaskazini wakisema wanajeshi wa Uganda wanakaribishwa nchini Kongo ili kuwatokomeza waasi wa kundi la ADF la waislamu wenye itikadi kali. Die tageszeitung linasema kwa muda mrefu wanajeshi  wa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo hawajachukua hatua zozote dhidi ya kundi la ADF na ndiyo sababu magaidi hao wameweza kuvamia vijiji na kuwaua raia mara kwa mara.

Vyanzo: Deutsche Zeitungen