1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika Katika Magazetini ya Ujerumani wiki hii

Oumilkheir Hamidou
7 Oktoba 2016

Mkutano wa kunusuru mimea na viumbe wanaokabiliwa na hatari ya kutoweka mjini Johannesburg, sababu zinazowafanya vijana wa Afrika kukimbilia Ulaya na zana za kimambo leo kutahiri vijana Afrika kusini magazetini

https://p.dw.com/p/2R16l
Nembu ya mkutano wa kuhifadhi maisha ya wanyama na mimea adimu
Nembu ya mkutano wa kuhifadhi maisha ya wanyama na mimea adimuPicha: DW/B. Bascomb

 

Tuanzie lakini Johannesburg,Afrika Kusini ambako wiki iliyopita ulimalizika mkutano wa  kimataifa kuhusu namna ya kunusuru mimea na maisha ya viumbe wanaokabiliwa na hatari ya kutoweka. Mkutano huo ulioanza wiki mbili kabla umemalizika jumatano iliyopita kwa kufikiwa makubaliano yaliyosifiwa na wanaharakati wanaopigania mazingira walioyataja kuwa" ni ya kihistoria."Baadhi ya vifungu vya makubaliano hayo yaliyofikiwa na mataifa 183 vinaweza kudhamini maisha ya viumbe vilivyoko hatarini,yasiangamie.

"Matumaini mepya" ndio kichwa cha maneno cha gazeti la Der Tagesspiegel" linalolalamika hata hivyo kwamba baadhi ya visa vya kikatili mfano wa "uwindaji wa kikatili" wa simba katika viunga vya Afrika Kusini. Katika hatua dhidi ya "kuteketezwa misitu ya joto" linaandika gazeti la Der Tagesspiegel, mataifa yamekubaliana kuiwekea vizuwizi biashara ya zaidi ya aina 300 ya mbao za misitu ya joto. Mbali na tumbili wa Berber-aina pekee ya kima wanaokutikana Ulaya, kuna aina nyengine za wanyama wanaokabiliwa na hatari ya kutoweka ulimwenguni ambao pia watahifadhiwa sawa na aina fulani ya papa wanaokabiliwa na hatari ya kutoweka."Tumefanikiwa kuleta mageuzi ya kweli katika mtazamo wa wajumbe mkutanoni " amenukuliwa na gazeti la Der Tagesspiegel  Kelvin Alie wa shirika linalopigania kinga ya wanyama IFAW.

Wanyama pori wanazigawa nchi za Afrika

Gazeti hilo linazungumzia pia majadiliano makali yaliyozuka Johannesburg kuhusu hifadhi ya ndovu wa kiafrika. Zimbabwe na Namibia zimeshindwa katika juhudi zao za kutaka waruhusiwe kuuza shehena ya pembe za ndovu walizo nazo. Der Tagesspiegel limezitaja pia tofauti zilizojitokeza kati ya wanaounga mkono msimamo wa mashirika ya magharibi ya kupigania hifadhi za mimea na wanyama wanaokabiliwa na hatari ya kutoweka na wale wanaoyapinga mashirika hayo ya magharibi wanaohisi wanataka kulazimisha sheria zao. Mkutano kuhusu hufadhi ya wanyama na mimea inayokumbwa na hatari ya kutoweka umefichua ufa katika Umoja wa nchi za Afrika,linamaliza kuandika gazeti la Der Tagesspiegel.

 Ziara ya Kansela Angela Merkel nchini Mali,Niger na Ethiopia

 

Mada nyengine iliyogonga vichwa vya habari za magazeti ya Ujerumani kuhusu Afrika wiki hii inahusu wimbi la waafrika wanaokimbilia Ulaya.Gazeti la Handelsblatt linaandika katika uhariri wake na kusema Ulaya haizijui sababu zinazopelekea mikururo ya waafrika kuja ulaya.Tangu ilipofungwa njia ya Balkan mwezi March uliopita,mikururo ya wakimbizi kutoka kusini mwa dunia haijapungua,wanafuata njia nyengine. Maelfu ya wakimbizi,wengi wao wa Afrika,wanaondokea katika eneo la mwambao wa Misri na kuelekea kaskazini-wanasafiria mashua ambazo hata havifai kusafiria.

Handelsblatt linazungumzia ripoti zilizohanikiza katika vyombo vya habari vya Ujerumani kuhusu misiba inayotokea baharini, na miito ya kudai sera za huruma zaidi kwa wakimbizi -Handelsblatt limezungumzia pia pendekezo la serikali kuu ya Ujerumani kuzidisha kiwango cha misaada ya maaendeleo. Suala la wimbi la wakimbizi ,linaendelea kuandika gazeti la Handelsblatt litakuwa mojawapo ya mada ambazo kansela Angela Merkel atazizungzia katika ziara yake ya siku tatu inayoanzia leo jumapili  na ambayo itamfikisha pia katika makao makuu ya Umoja wa Afrika mjini Addis Abeba nchini Ethiopia. Kiroja ni kwamba macho ya magharibi ni nadra kulengwa katika zile nchi ambako wakimbizi wanatokea-kawaida linaendelea kuandika gazeti hilo wangebidi kuelekeza macho kwanza katika nchi hizo ili kujua chanzo cha mzozo wa wakimbizi badala ya kumimina fedha kwa pupa kugharimia miradi ambayo si sana kufanikiwa.

Gazeti la Handelsblatt linavikosoa pia vyombo vya habari vya Afrika ambavyo gazeti hilo la mjini Düsseldorf linasema havizungumzii vya kutosha kuhusu wakimbizi. Badala ya kukosoa "senyenge na kuta zinazozungushwa ulaya" vyombo vya habari vya Afrika vingepaswa pia kuuliza Umoja wa Afrika kwanini haujawahi hata mara moja kuitisha mkutano kuzungumzia tatizo la wakimbizi? Linamaliza kuandika gazeti la Handelsblatt.

Zana za kimambo leo vya kutahiri vijana Afrika Kusini

Na mada ya mwisho magazetini inahusiana na kuvumbuliwa zana za aina mpya za kuwatahiri vijana wa Afrika Kusini badala ya mitindi ya zamani ambayo gazeti la Neues Deutschland linasema imekuwa ikiwasumbua watoto wa Mandela

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/BASIS/PRESSEM/ALL/PRESSE

Mhariri:Yusuf Saumu