1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Al-Shabaab yauwa tena Mandera

Daniel Gakuba
25 Oktoba 2016

Wiki tatu baada ya kuuwa watu sita katika mji wa Mandera ulio kaskazini mashariki mwa Kenya, kundi la kigaidi la al-Shabaab lashambulia tena na kuuwa watu 12 kwenye mji huo likitumia mabomu na bunduki.

https://p.dw.com/p/2Rfpu
Kenia Anschlag in der Stadt Mandera
Picha: picture-alliance/AP Photo

Kundi la kigaidi la al-Shabaab kutoka Somalia limedai kuhusika na mashambulizi hayo, likidai kupitia kituo chake cha redio cha Andalus, kwamba waliouawa ni 15.

Chanzo cha polisi kimeliambia shirika la habari la AFP kuwa waliopoteza maisha ni wanaume 11 na mwanamke mmoja, waliokuwa katika nyumba ya wageni ya Bisharo katika Kaunti ya Mandera.

Hii ni mara ya pili kwa al-Shabaab kufanya mashambulizi katika Kaunti ya Mandera katika muda wa wiki tatu. Mashambulizi mengine ya tarehe 6 mwezi huu wa Oktoba yaliuawa watu sita katika jengo ambalo linakaliwa zaidi na watu wasiokuwa na asili ya Kisomali na wasiokuwa Waislamu.

Taarifa za hivi punde zimeeleza kuwa al-Shabab imefanya mashambulizi mengine katika kambi ya walinzi wa amani wa Umoja wa Afrika katika eneo la Baledweyne nchini Somalia.