1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rwanda yalalamika kuchafuliwa sifa na wakimbiza wakikongo

Saumu Mwasimba
22 Februari 2019

Zaidi ya wakimbizi  60 raia wakongo wamekamatwa kwa kusababisha kutolewa maoni ya ukosoaji na jumuiya ya Kimataifa dhidi ya Rwanda. Wakimbizi hao pia wameshtakiwa kwa kosa la kusababisha vurugu dhidi ya maafisa wa umma.

https://p.dw.com/p/3DsqF
Ruanda Kiziba Flüchtlingslager
Picha: Getty Images/AFP/S. Aglietti

Maafisa wa polisi  waliowafyetulia risasi wakimbizi raia wa kongo waliokuwa wakiandamana kupinga punguzo la msaada waliokuwa wakipata lazima wachunguzwe na kubebeshwa dhamana limesema shirika la Amnesty International lenye makao yake mjini London Uingereza ,ikiwa ni mwaka mmoja baada ya kiasi wakimbizi 11 kuuwawa katika makambi ya Karogi na Kiziba Magharibi mwa Rwanda.

Kutokana na kutochapishwa rasmi kwa uchunguzi wowote wa maouaji ya waandamanaji hao,kiasi wakimbizi 63 wanakabiliwa na mashataka wakihusishwa na maandamano hayo ambayo yanajumuisha kushiriki katika maandamano yasiyokuwa halali dhidi ya serikali ya Rwanda.

Waandamanaji hao pia wanashtakiwa kwa kusababisha vurugu dhidi ya maafisa waserikali. Sarah Jackson ambaye ni naibu mkurugenzi wa Amnesty International anayehusika na eneo la pembe ya Afrika na maziwa makuu anasema badala ya utawala wa Rwanda kuwatuhumu wakimbizi wakikongo kwa kuwaharibia sura nchi yao maafisa wa nchi hiyo wanapaswa kuchunguza jinsi wakimbizi walivyoishia kuwawa wakati wa maandamano yaliyokuwa yakilindwa na maafisa wa polisi na kuwabebesha jukumu waliohusika na mauaji hayo.

Ripoti ya Shirika hilo la Amnesty  juu ya mauaji ya wakimbizi hao imelaani hatua ya kukosekana uchunguzi katika tabia za maafisa wa polisi waliotumia nguvu kubwa kupita kiasi dhidi ya wakimbizi katika kambi ya Umoja wa Mataifa chini ya shirika la kuwahudumia wakimbizi UNHCR katika maeneo ya Karogi na Kiziba  tarehe 22 Februari mwaka jana.

Flüchtlingslager Kigeme in Ruanda
Picha: AFP/Getty Images

Inatajwa kwamba Februari 20 mamia ya wakimbizi raia wakongo walitembea kwa miguu umbali wa kilomita 15 kutoka kambi ya Kiziba wakiandamana kupinga kupunguziwa msaada waliokuwa wakipokea kutoka UNHCR wakidai ama kurudishwa kwao Kongo au kuhamishiwa nchi nyingine.Pamoja na kutakiwa kusitisha maandamano hayo na polisi,maafisa wa serikali wa eneo hilo na wafanyakazi wa UNHCR walishikilia msimamo wao na kuendelea kuandamana lakini mnamo tarehe 22 Februari polisi waliamua kutumia gesi ya kutowa machozi kuwatawanya na kufyetua  risasi za moto ambapo wakimbizi wanane waliuwawa papo hapo na wengine chungunzima walijeruhiwa huku watatu walikufa kambini siku hiyohiyo kufuatia majeraha..

Kutokana na suala hilo shirika la Amnesty International sasa linaitaka serikali ya Rwanda kuanzisha uchunguzi huru na usio pendelea kuhusu tabia ya jeshi lake la polisi katika matumizi ya nguvu kubwa kupita kiasi bila ya sababu ya msingi kuwatawanya waandamanaji hao. Shirika hilo linatowa mwito kwamba uchunguzi lakini uanzishwe kubaini ikiwa matumizi ya nguvu yalikuwa na ulazima na kiwango cha nguvu iliyotumiwa ikiwa imekwenda na kanuani za haki za binadamu ya nchini Ruanda. Lakini pia shirika hilo limetaka kwamba wakati uchunguzi huo ukifanyika maafisa husika katika tukio hilo wanapaswa kusimamishwa kazi ikiwa kunhja ushahidi wa kutosha wote waliohusika wanalazimika kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria kujibu kesi.

Mwandishi:Saumu Mwasimba

Mhariri: Iddi Ssessanga