1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ANC kinaongoza matokeo ya uchaguzi licha ya kula hasara

Oumilkheir Hamidou
10 Mei 2019

Ushindi wa chama cha African National Congress, ANC, katika uchaguzi wa bunge nchini Afrikia Kusini unazidi kuthibitika. Hata hivyo kwa mara ya kwanza katika historia ya chama hicho, wamepata chini ya asilimia 60.

https://p.dw.com/p/3IHE4
Südafrika Parlamentswahl Stimmauszählung
Picha: Reuters/R. Ward

Baada ya kuhesabiwa asilimia 80 ya kura ANC, kimejipatia asiliamia 56.99. Kimepoteza nukta  takriban tano ikilinganishwa na matokeo ya uchaguzi wa mwaka 2014. Pindi matokeo hayo yakithibitika, basi yatakuwa mabaya kabisa kwa chama hicho cha Nelson Mandela katika uchaguzi wa bunge. Chama cha upinzani cha Democratic Alliance kimejikingia hadi sasa asili mia 21.83  huku chama cha siasa kali za mrengo wa kushoto - Wapigania Uhuru wa Kiuchumi , EFF, wanaoongozwa na Julius Malema wamejikingia asili mia 10.01.

"Nimeridhika vya kutosha", amesema  mwenyekiti wa Democratic Alliance, Mmusi Maimane jana usiku.

Hata hivyo, ANC kinatarajiwa kuendelea kudhibiti wingi mkubwa wa viti katika bunge lenye viti 400 na Cyril Ramaphosa kuchaguliwa na wabunge kuendelea na wadhifa wake wa rais wa Afrika Kusini.

Viongozi wa ANC hadi wakati huu wamejizuwia kusema chochote kuhusu matokeo hayo au kusherehekea ushindi."Tutaunda serikali inayokuja" , naiwe tumepungukiwa au tumepata kura zaidi" amesema mmojawapo wa viongozi hao, Gwede Mantashe.

Cyril Ramaphosa katika kampeni zake za uchaguzi
Cyril Ramaphosa katika kampeni zake za uchaguziPicha: DW/A. Kriesch

Cyril Ramaphosa hakufanikiwa kutekeleza ahadi alizotoa mwaka mmoja uliopita

Ramaphosa amepangiwa kwenda Pretoria kukitembelea kituo cha tume ya uchaguzi, ambako ndiko kura zinakohesabiwa."ANC kinaelekea  kupata ushindi madhubuti tukilinganisha na matokeo finyu ya utawala wake" amesema kwa upande wake mdadisi Daniel Silke.

LIcha ya umaarufu, Cyril Ramaphosa hakuweza kupunguza hasara.Tangu alipoingia madarakani mapema mwaka 2018 amekua akiahidi "kurekebisha makosa ya chama chake, kupiga vita rushwa na kuinua uchumi. Mwaka mmoja baadaye, kiongozi huyo wa zamani wa chama kikuu cha wafanyakazi wa Afrika Kusini hakufanikiwa kutekeleza ahadi zake. Katika kipindi chote cha kampeni zake za uchaguzi alikuwa akikabiliana na maudhi na hasira za watu waliochoshwa na rushwa, ukosefu wa ajira na pia ukosefu wa hali ya usawa, miaka 25 baada ya kutoweka enzi za ubaguzi wa rangi na mtengano Apartheid.

Kutokana na matokeo finyu ya uchaguzi, wadadisi wengi wanaashiria Cyril Ramaphosa atakabiliana na shida ya kuhakikisha miradi yake ya mageuzi inaidhinishwa hasa kwakua ndani ya chama cha ANC bado kuna wale wanaomuunga mkono rais wa zamani Jacob Zuma.

 Matokeo rasmi ya uchaguzi yanatarajiwa Jumamosi na Rais Cyril Ramaphosa ataapishwa rasmi Mei 25 inayokuja.

Chanzo: Reuters