Asasi za kiraia zahofia ghasia kutokea DRC
20 Desemba 2018Asasi nyingi za kiraia zinahofia ghasia na machafuko siku zijazo nchini DRC kutokana na hatua ya kuahirisha uchaguzi.
Katika tangazo lililo sambazwa katika vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, uratibu wa asasi za kiraia eneo la Kivu kusini unasema kutokubaliana na hatua ya kuahirisha tarehe ya uchaguzi kutokana na jinsi uchaguzi huo ulivyowahi kuahirishwa mara nyingi hapo awali kabla ya kalenda ya uchaguzi kutangazwa. Patient Bashombe ambaye ni kiongozi wa asasi za kiraia amesema iwapo kweli uchaguzi huu utaahirishwa huenda ghasia zikaongezeka kabla ya kufikia tarehe hiyo.
Patient Bashombe amewatolea mwito raia wa Congo pamoja na Umoja wa Mataifa kuongeza msukumo ili viongozi wa serikali pamoja na tume ya uchaguzi CENI iandae uchaguzi huo kama ilivyopangwa yaani tarehe 23 Jumapili.
Upande wa wakaazi wanazungumzia masikitiko yao kwa sababu walishajiandaa kimawazo kushiriki kwenye uchaguzi huo Jumapili Desemba 23.
Hadi sasa, wagombea wanaofanya kampeni wanazidi kujiuliza ikiwa kampeni itaendelea pia au itasitishwa sababu hawana uwezo wa kuendelea na kampeni.
Mitima Delachance, DW, Bukavu