1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Assad aonya kuhusu vita vya Syria

Grace Kabogo
11 Mei 2018

Rais wa Syria, Bashar al-Assad ameyalinganisha mapigano yanayoendelea nchini mwake na ''vita vya dunia'' na ameonya kuhusu hatari ya kutokea mzozo wa moja kwa moja kati ya mataifa yenye nguvu yanayohusika na vita hivyo.

https://p.dw.com/p/2xVuo
Syrien Bashar Assad im Interview in Damaskus
Picha: picture-alliance/AP Photo/SANA

Rais Assad ameitoa kauli hiyo katika mahojiano na gazeti moja la Ugiriki na kusema kuwa mapigano ya Syria ni zaidi ya 'vita baridi'. Kwenye mahojiano hayo, kiongozi huyo wa Syria amezungumzia masuala kadhaa ikiwemo shutuma za mashambulizi ya silaha za sumu, majeshi ya Marekani nchini Syria na uwezekano wa yeye kujiuzulu kama suluhisho la kisiasa la mzozo huo uliodumu kwa miaka saba.

Akijibu swali kuhusu matumizi ya silaha za sumu, Assad amesema nchi yake inayaheshimu maazimio ya Umoja wa Mataifa na ilikabidhi akiba ya silaha zake ilizokuwa imezihifadhiwa kwa mamlaka za kimataifa na kwamba Syria haina silaha za sumu.

''Hatuna silaha zozote za sumu tangu tulivyoachana nazo mwaka 2013 na Shirika la kimataifa la kuzuia kuenea kwa silaha za kemikali limefanya uchunguzi wake kuhusu hili na hali inajieleza wazi kwamba hatuna hizo silaha,'' alisema Assad.

Tel Aviv Netanjahu PK Iran Atomprogramm (picture alliance / Photoshot)
Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin NetanyahuPicha: picture-alliance/Photoshot

Wakati hayo yakijiri, Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu amesema mashambulizi ya mabomu dhidi ya Iran nchini Syria yalikuwa sahihi kwa ajili ya kujibu mashambulizi ya roketi yaliyofanywa na vikosi vya Iran. Netanyahu amethibitisha kuwa Israel ilikuwa ikivilenga vikosi vya Iran nchini Syria, baada ya Iran kushambulia katika milima ya Golan inayodhibitiwa na vikosi vya Israel. Amesema Israel haitoiachia Iran iwe na nguvu nchini Syria.

Awali jeshi la Israel lilivishutumu vikosi vya Iran kwa kurusha makombora 20 yaliyoilenga milima ya Golan, eneo la mpaka ambalo liliwahi kutawaliwa na Syria, lakini linadhibitiwa na Israel kwa zaidi ya miaka 50. Baadhi ya makombora yalizuiwa na mfumo wa kujikinga na makombora wa Israel.

Ardhi ya Israel haijashambuliwa

Jeshi limesema hakuna mtu yeyote aliyeuawa au kujeruhiwa na hakuna makombora yaliyoshambulia katika eneo la Israel. Aidha, Israel imelitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kulaani mara moja shambulizi hilo. Iran kwa upande wake imekanusha kuhusika na mashambulizi hayo ya roketi na imelaani vikali mashambulizi yaliyofanywa na Israel. Pia imeunga mkono hatua hiyo ya Syria ikisema nchi hiyo ina haki ya kujilinda yenyewe, na imeishutumu jumuiya ya kimataifa kwa kuyafumbia macho mashambulizi yanayofanywa na Israel dhidi ya mshirika wake muhimu.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres ametoa wito wa kusitishwa mara moja vitendo vyovyote vya kiuchokozi ili kujiepusha na mgongano mpya katika Mashariki ya Kati.

Den Haag Schlusszeremonie des UN-Kriegsverbrechertribunals für Ex-Jugoslawien | UN-GeneralSekretär Antonio Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio GuterresPicha: Reuters/United Photos/T. Kluiters

Msemaji wa Guterres, Stephane Dujarric amesema kikosi cha kulinda amani cha umoja huo katika milima ya Golan kimeendelea kuwasiliana na jeshi la Syria na Israel na kuzihimiza pande zote kujizuia na mashambulizi na kuheshimu makubaliano ya mwaka 1974 ya kusitisha mapigano.

Hata hivvyo, hadi asubuhi ya leo hakuna mwanachama yeyote wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambaye ameitisha mkutano. Baraza hilo limegawanyika vibaya kutokana na mzozo wa Syria.

Mwandishi: Grace Patricia Kabogo/DPA, AP, AFP, Reuters, DW https://bit.ly/2KRwHfT
Mhariri: Iddi Ssessanga