1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Australia kuimarisha sheria dhidi ya ugaidi

24 Septemba 2014

Bunge la Australia leo limewasilisha muswada wa sheria kali za kupambana na ugaidi, ambapo itakuwa ni uhalifu kwa mtu kusafiri kwenda maeneo yanayozingatiwa kuwa ya kigaidi.

https://p.dw.com/p/1DJcm
Al-Nusra Front Kämpfer in Syrien 22.09.2014
Picha: AFP/Getty Images/Rami Al-Sayed

Mabadiliko yanakuja huku serikali ikisema takribani raia 60 wa nchi hiyo wamekwenda Iraq na Syria kupigana upande wa wanamgambo wenye itikadi kali na huenda wakarejea nyumbani na kuzusha machafuko.

Mswada huo uliopewa jina la Mabadiliko ya Sheria ya Kupambana na Ugaidi wa Wapiganaji wa Kigeni unapendekeza kuwa itakuwa ni kinyume cha sheria kuingia au kusalia katika kile kinachojulikana kama “eneo lililotangazwa, ambalo waziri wa mambo ya kigeni ataridhika kuwa kundi la kigaidi linajihusisha na harakati za kivita.

Sheria hiyo haitamzuia mtu anayesafiri katika eneo kama hilo kwa sababu halali kama vile kutoa msaada wa kiutu, kwa niaba ya serikali ya Australia au Umoja wa Mataifa, kuripoti kuhusu matukio au kuitembelea familia yake, lakini inasema kuwa “wale wanaosafiri katika eneo lililotangazwa bila kuwa na sababu halali huenda wakajihusisha katika kitendo cha uadui dhidi ya Australia na kundi lililoorodheshwa kuwa la kigaidi". Na watu hao kisha wanaweza kurudi nyumbani wakiwa na uwezo wa kutosha wa kutumiwa kujihusisha na matendo ya kigaidi au uhalifu mwingine nchini Australia. Kosa hilo litabeba adhabu ya juu ya kifungo cha hadi miaka 10 jela.

Melbourne Australien Polizei erschießt Terrorverdächtigen 24.9.2014
Polisi mjini Melbourne walimpiga risasi na kumuua mshukiwa wa ugaidi aliyewashambulia polisiPicha: picture-alliance/dpa

Hayo yanajiri baada ya polisi mjini Melbourne kumpiga risasi na kumuua “mtuhumiwa wa ugaidi” ambaye aliwachoma kisu polisi wawili, siku moja baada ya kundi la Dola la Kiislamu kuwataka waislamu kuwauwa Waustralia.

Tony Abbott ni waziri Mkuu wa Australia. Mabadiliko hayo ya sheria yatawasilishwa kwenye kamati ya ujasusi ya bunge ili kutathminiwa na watakuwa na muda wa hadi Oktoba 17 kufanya maamuzi. Muswaada huo pia unasema ni hatia “kuutetea ugaidi” na adhabu yake inaweza kuwa hadi miaka mitano gerezani. Mwanasheria mkuu George Brandis amesema mabadiliko hayo yanaangazia “mianya ambayo imekuwepo katika sheria ya kupambana na ugaidi nchini Australia, na hasa kuhusiana na vitisho vinavyowekwa na wapiganaji makundi ya kigaidi wanaorejea nyumbani kutoka maeneo ya vita.

Msemaji wa chama cha upinzani cha Labor, Mark Dreyfus, anasema chama chake uko tayari kuunga mkono baadhi ya mabadikiko hayo, ikiwa ni pamoja na pendekezo la kuzuia kwa muda paspoti za watu ili kuwazia kujiunga na migogoro inayoendelea nchini Syria na Iraq.

Lakini amesema kuna masuala mengine, yakiwemo yanayohusiana na kile kinachofahamika kama maeneo yanayozingatiwa kuwa ya ugaidi, ambayo amesema siyo ya kawaida katika katiba ya Australia na yanayohitaji uchunguzi wa kina.

Muungano wa mawakili nchini Australia umeyakosoa baadhi ya mabadiliko hayo, ukisema raia waliosafiri katika maeneo kama nchini Syria na Iraq huenda wakachukuliwa kuwa na mahusiano na mitandao ya kigaidi, kama hawataweza kuthibitisha mahakamani kuwa hawana hatia punde wanaporejea nyumbani.

Mawakili pia wanasema muswaada huo unaopendekezwa pia unaweza kuwapa polisi mamlaka makubwa ya kuwakamata na kuwazuilia raia wa Australia ili kuzuia kitendo cha ugaidi.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Mohammed Khelef