1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marufuku ya Umoja wa Ulaya kwa wanasiasa wa Uturuki

5 Machi 2017

Kansela wa Austria Christian Kern amesema Jumapili (05.02.2017) wanasiasa wa Uturuki wanapaswa kupigwa marufuku kufanya kampeni za kisiasa katika nchi zote za Umoja wa Ulaya.

https://p.dw.com/p/2Yfoc
Christian Kern
Kansela Christian Kern wa Austria.Picha: Getty Images/AFP/J. Thys

Kern ameliambia gazeti la Ujerumani la Welt am Sonntag kwamba "Jibu la pamoja la Umoja wa Ulaya kuzuwiya kampeni hizo litakuwa na maana ili kwamba nchi binafsi kama vile Ujerumani ambapo wanakatazwa kujitokeza katika kampeni hizo haziishii kushinikizwa na Uturuki".

Kiongozi wa Austria ameliambia gazeti hilo la Welt am Sonntag kwamba mazungumzo yanayofanyika kwa muda mrefu na Uturuki kutaka kujiunga na Umoja wa Ulaya yanapaswa kuahirishwa kutokana na hatua ya Rais Erdogan wa Uturuki kuzikanyaga haki za binaadamu na haki za msingi za kidemokrasia.

Kern amesema hawawezi kuendelea kuzungumzia kuhusu uwanachama na nchi ambayo kwa miaka mingi imekuwa ikijitenganisha na maadili ya demokrasia na kanuni za utawala wa sheria.Anaona kwamba kuanzishwa kwa mfumo wa urais nchini humo utakaokuwa na madaraka makubwa kutazidi kudhoofisha utawala wa sheria,kupunguza kutenganishwa kwa madaraka na kutakwenda kinyume na maadili ya Umoja wa Ulaya.

Uturiki yapigania hura ya ndio

Türkei Erdogan wirft Deutschland «Nazi-Praktiken» vor
Rais Tayyip Erdogan wa Uturuki.Picha: Reuters/M. Sezer

Serikali ya Uturuki imekuwa ikijaribu kuwavutia wapiga kura miongoni mwa Wajerumani milioni tatu wenye asili ya Kituruki ambayo ni idadi kubwa ya Waturuki wanaoishi nje ya nchi hiyo kuunga mkono kuongezewa madaraka kwa Rais Tayyip Erdogan wakati kura ya maoni itakapopigwa hapo tarehe 16 Aprili.

Miji kadhaa ya Ujerumani ilizuwiya kujitokeza kwa mawaziri wa serikali ya Erdogan wiki iliopita kwa kile ilichosema sababu za usalama.Kuahirishwa kwa mikutano hiyo ya hadhara kuliikasirisha serikali ya Uturuki ambayo imeituhumu serikali ya Ujerumani kwa kutaka kuiyumbisha kampeni yake ya kura ya maoni.

Hapo Jumamosi Kansela Angela Merkel wa Ujerumani alimpigia simu Waziri Mkuu wa Uturuki Binali Yildrim kujaribu kuuzima mzozo huo na mawaziri wa mambo ya nje wa nchi hizo mbili wanatazamiwa kukutana baadae wiki hii.

Italien Außenminister Gabriel in Rom
Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Sigmar Gabriel.Picha: picture-alliance/abaca/R. De Luca

Ujerumani kutetea utawala wa sheria

Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Sigmar Gabriel katika makala ya mgeni kwenye gazeti la Ujerumani la Bild am Sonntag amesema "kwa hakika hawatoacha kukosowa kwa matukio yanayoendelea Uturuki".

Gabriel amesisitiza kwaba Ujerumani itasimama kidete kutetea utawala wa sheria,uhuru wa kutowa maoni,haki za binaadamu na demokrasia.

Amepinga kukamatwa kwa mwandishi wa gazeti la Die Welt la Ujerumani Deniz Yücel kwa madai ya ugaidi kuwa sio sahihi na kumepindukia kiwango.Amesema uhusiano wa kirafiki kati ya Ujerumani na Uturuki na mzito kuliko mvutano wa kidplomasia wanopitia hivi sasa.

Mwandishi : Mohamed Dahman /AFP

Mhariri : John Juma