1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bado mshukiwa wa mauaji Ufaransa asubiriwa kujisalimisha

MjahidA21 Machi 2012

Mtu aliyejitambulisha kama muasi aliyejifungia katika nyumba moja mjini Toulouse nchini Ufaransa baada ya misururu ya mashambulizi ya risasi sasa ameanza tena kuwasiliana na polisi

https://p.dw.com/p/14Ojz
Polisi mjini Toulouse wakizunguka nyumba ya mshukiwa
Polisi mjini Toulouse wakizunguka nyumba ya mshukiwaPicha: dapd

Mtu huyo anashukiwa kuwa ndiye aliyewauwa watu wanne katika shule moja ya Wayahudi Jumatatu iliopita pamoja na mauaji ya hapo kabla ya wanajeshi watatu wenye asili ya Afrika kaskazini.

Kulingana na maafisa wa polisi nchini humo mshukiwa Mohammed Merah aliye na umri wa miaka 23 na raia wa Ufaransa mwenye asili ya Algeria, aliyejigamba kuwa na mafungamano na kundi la kigaidi la Al Qaeda alikuwa amekatiza mawasilianao na polisi kwa muda wa masaa mawili. Merah ambaye kwa sasa ameanza tena mawasiliano na polisi alisema alifanya mauaji hayo kulipiza kisasi kutokana na mauaji ya watoto wa kipalestina.

Waziri wa ndani wa Ufaransa Claude Gueant amesema polisi wawili wa kitengo maalum walijeruhiwa walipojaribu kuvamia nyumba ya Maher ilio Kusini Magharibi mwa nchi hiyo. Waziri huyo amesema awali mshukiwa aliyejihami kwa silaha nzito aliahidi kujisalimisha kwa polisi hii leo.

Rais wa Ufaransa Nicolas Sarkozy
Rais wa Ufaransa Nicolas SarkozyPicha: dapd

Zoezi la kumsaka mshukiwa wa mashambulizi ya mara kwa mara nchini Ufaransa lilianzishwa baada ya wiki tatu ya mashambulizi katika siku tisa zilizopita ambapo mtu anayeendesha pikipiki anaaminika kufanya mashambulizi hayo na kusababisha vifo vya watu tisa wakiwemo watoto watatu wa kiyahudi na wanajeshi watatu ambao hawakuwa kazini katika eneo la Toulouse.

Ufaransa laazima iungane pamoja

Rais wa Ufaransa Nicolas Sarkozy amefika katika eneo ambalo polisi wamelizingira kwa zaidi ya saa 11 wakiwa na matumaini ya mshukiwa huyo kujisalimisha kwao. Rais Sarkozy alikuwa anatarajiwa kuzungumza na mkuu wa polisi anayesimamia shughuli hiyo, mjini Toulouse pamoja na wawakilishi wa dini kabla ya kwenda kuwaona majeruhi wa shambulio la Jumatatu hospitalini. Rais huyo wa Ufaransa pia anatarajiwa kuhudhuria hafla ya kutoa heshima za mwisho kwa wanajeshi waliouawa.

"Tunabidi tuungane, tusiachie kushawishiwa na uchochezi wala kisasi. Kutokana na tukio kama hili ukubwa wa taifa la ufaransa utajitokeza tu tukiwa kitu kimoja, ni wajibu wetu mbele ya marehemu waliouliwa kinyama na ni wajibu wetu kwa nchi yetu" Alisema Rais Sarkozy.

Kwa upande wake afisa mmoja katika idara sheria nchini humo amesema mamake mshukiwa, kakake pamoja na rafiki wa kike wa kakake yake walizuiliwa ili kuhojiwa.

Wakati huo huo katika mji mkuu i Paris bomu moja liliripuka leo katika ubalozi wa Indonesia na kusababisha madhara madogo.

Polisi mjini humo wamesema hakuna mtu yoyote aliyejeruhiwa. Duru ya wizara ya nje ya Indonesia imesem kwa sasa ni mapema mno kusema kama kuna mafungamano kati ya shambulizi hilo na yale yaliofanyika kusini mwa Ufaransa.

Mwandishi: Amina Abubakar

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman