1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Baghdad.Jamii zatofautiana kuhusu hukumu ya kifo dhidi Sadam Husein.

6 Novemba 2006
https://p.dw.com/p/CCvP

Mji mkuu wa Iraq, Baghdad bado umebakia katika hali ya watu kutotoka nje baada ya siku moja ya kutangazwa hukumu ya kifo kwa Rais wa zamani wa nchi hiyo Saddam Hussein, kutokana na kosa la uhalifu dhidi ya ubinaadamu.

Hapo jana kiongozi huyo wa zamani wa Iraq alihukumiwa kunyongwa hadi kufa kufuatia mauaji ya watu 148 katika kijiji cha Washia katika mji wa Dujail mnamo mwaka 1982.

Maamuzi hayo yamepokelewa kwa mitazamo tofauti nchini Iraq huku dunia ikiwa na wasi wasi kuwa kutekelezwa kwa hukumu hiyo kutapelekea maafa zaidi nchini humo.

Waziri mkuu wa Iraq, Nouri al-Maliki amesema kuwa, Saddam Hussein alikuwa ni muuaji anaestahiki adhabu hiyo aliyopewa, wakati Rais wa Marekani George W. Bush ameeita adhabu ya kifo kwa Saddam kuwa ni njia ya kuelekea demokrasia.

Hata hivyo viongozi kadhaa wa Ulaya wanakubali makosa aliyoyafanya Rais huyo wa zamani wa Iraq, lakini hawakubaliani na hukumu ya kifo iliyopitishwa.

Waziri mkuu wa Uingereza Tony Blair amesema

“Kesi ya Saddam Husein imetupa fursa ya kujionea kilichotokea zamani nchini Iraq, matumizi ya nguvu, udhalimu, malaki ya watu kuuwawa na vita vilivyosababisha hasara ya milioni kadhaa. Na imesaidia pia kufungua njia ya kupatikana kile wananchi wa Iraq wanachokitaka nacho ni kuwa na nchi ambyo jamii zote zitaweza kuishi kwa amani na kujiamulia wenyewe mustakbali wao kwa njia za kidemokrasi“.