1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bandari ya Sirte yakombolewa

11 Juni 2016

Vikosi washirika wa serikali ya umoja wa kitaifa nchini Libya vimesema Jumamosi (11.06.2016) vimeikombowa bandari kutoka ngome kuu ya wapiganaji wa kundi la Dola la Kiislamu waliozingirwa ndani ya mji wa Sirte.

https://p.dw.com/p/1J4wl
Picha: picture-alliance/ZUMA Press/H. Turkia

Kutekwa kwa Sirte mji alikozaliwa dikteta aliyeon'golewa madarakani Moamer Gaddafi litakuwa pigo kubwa kwa wapiganaji hao wa itikadi kali ambao tayari wamepoteza maeneo waliyokuwa wakiyashikilia nchini Syria na Iraq ambapo wamejitangazia utawala wa khalifa yaani wa Kiislamu.

Vikosi hivyo vya Libya pia vimeyakombowa maeneo ya wakaazi mashariki mwa mji huo wa Sirte ambao kwa mwaka mmoja uliopita ulikuwa kambi kuu ya kundi la Dola la Kiislamu katika nchi hiyo ya Afrika Kaskazini.

Msemaji wa vikosi hivyo Rida Issa ameliambia shirika la habari la AFP kwamba wapiganaji hao hivi sasa wamezingirwa wakiwa kwenye eneo lenye idadi kubwa ya watu la kama kilomita tano za mraba ndani ya mji huo ambapo wamekuwa wakitega mabomu.Amesema takriban wakaazi wengi wa mji huo wamekimbia na ni 30,000 tu waliobakia.

Ushindi wa kushangaza

Kufuatia operesheni ya mwezi mmoja ya kuujongelea mji huo kusonga mbele kwa haraka kwa vikosi hivyo washirika wa serikali ya Makubaliano ya Taifa ya (GNA) ambavyo vimeingia kwenye mji huo hapo Jumatano kumewashangaza maafisa wengi nchini Libya.

Vikosi vya GNA katika mapambano ya Sirte.
Vikosi vya GNA katika mapambano ya Sirte.Picha: picture alliance/abaca/H. Turkia

Afisa mmoja wa serikali amenukuliwa akisema mapambano hayakuwa makali kama vile walivyokuwa wakitarajia. Mjumbe wa Umoja wa Mataifa kwa Libya Martin Kobler amesema Jumamosi kupitia mtandao wake wa Twitter kwamba amevutiwa na hatua zilizopigwa kwa haraka na vikosi hivyo vya serikali ya Umoja wa Kitaifa (GNA ).

Mashirika ya ujasusi ya kigeni yanakadiria kwamba kundi hilo la Dola la Kiislamu lina wapiganaji wake 5,000 nchini Libya lakini nguvu zake ndani ya mji wa Sirte ambao kundi hilo la IS umekuwa ukiushikilia tokea Juni mwaka 2015 hazijulikani.Wapiganaji wa IS walijaribu kuirudisha tena mikononi mwake bandari ya mji huo hapo Jumamosi katika shambulio lililouwa wapiganaji wawili wa vikosi vya GNA.

Mapambano makali mitaani

Vikosi vya serikali ya umoja wa kitaifa nchini Libya vimekuwa na mapambano makali ya mitaani na wapiganaji wa jihadi karibu na kituo kikubwa kabisa cha mikutano wakati wa enzi ya Gaddafi ambacho kiliwahi huko nyuma kuwa na mikutano kadhaa ya kilele lakini hivi sasa kimekuwa makao makuu ya wanajeshi wa IS.

Jeshi la serikali katika viunga vya Sirte.
Jeshi la serikali katika viunga vya Sirte.Picha: picture alliance/Photoshot/(Xinhua/H. Turkia

Mwandishi wa shirika la habari la AFP ameripoti kuwepo kwa mapigano makali ya mitaani hapo Ijumaa kama kilomita mbili kutoka kituo hicho cha mikutano cha Ouagadougou.Vikosi vya GNA vilitumia vifaru, maroketi na mizinga wakati wapiganaji hao wa jihadi walijibu mapigo kwa bunduki za rashasha, mizinga na mashambulizi ya kuvizia.

Ndege zimefanya mashambulizi ya anga karibu na kituo cha mikutano na maeneo mengine ya IS mjini humo . Inaripotiwa kwamba wanajeshi 11 walio tiifu kwa GNA wameuwawa hapo Ijumaa na wengine 45 kujeruhiwa.

Serikali ya umoja wa kitaifa

Serikali ya GNA iliyoundwa kutokana na makubaliano ya kushirikiana madaraka yalioungwa mkono na Umoja wa Mataifa na kukubaliwa na baadhi ya wabuge wa Libya hapo mwezi wa Disemba imekuwa mbioni kusimamisha mamlaka yake lakini bado haikuidihinishwa rasmi na bunge linalalotambuliwa nchini humo.

Wapiganaji washirika wa serikali wakijongelea Sirte.
Wapiganaji washirika wa serikali wakijongelea Sirte.Picha: Reuters/Stringer

Vikosi vya GNA kwa kiasi kikubwa vinaundwa na wanamgambo kutoka miji ya magharibi hususan Misrata na walinzi wa vituo vya mafuta ambavyo IS mara kwa mara imekuwa ikijaribu kuvinyakuwa.

Vikosi washirika wa GNA vilisema hapo Alhamisi vinatarajia kutangaza kukombolewa kwa mji wa Sirte katika siku mbili tatu baada ya kujipenyeza kati kati ya mji huo.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AFP

Mhariri : Hamidou Oummilkheir