1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern Munich yakosa pointi 3 kuikaribia Schalke

12 Machi 2007

Laiti jana Bayern munich ingeondoka na pointi 3 badala ya sare ya 1:1 na Werder Bremen, ingekuwa pointi 4 tu nyuma ya viongozi wa Ligi Schalke.

https://p.dw.com/p/CHcY
Podolsko afumania lango la Bremen
Podolsko afumania lango la BremenPicha: AP

Mabingwa wa Ujerumani Bayern Munich walikosa jana nafasi bora kabisa ya kuziba mwanya kileleni kati yake na viongozi wa Ligi Schalke 04 walipomudu suluhu tu nyumbani ya bao 1:1 na Werder Bremen inayosimama nafasi ya pili.

Ilikua Lukas podolski alieufumania kwanza mlango wa Bremen mnamo dakika ya 7 ya mchezo ikionekana kana kwamba,Munich ingeondoka na ushindi mkuu.Lakini,Werder Bremen ikasema –kutangulia si kufika na mnamo dakika ya 66 ya mchezo Hugo Almeida alimvalisha kanzu kipa wa Munich Oliver kahn na mpira ukielekea katika lango lake Rosenberg akausindikiza kwa kichwa kuhakikisha unanasa wavuni.

Laiti ingelishinda na mkutoroka na pointi 3 jana, Bayern munich ingepunguza mwanya wake na Schalke hadi pointi 4.Sasa lakini wanabidim kuridhika na nafasi ya 4 ikiwa pointi 6 kutoka kileleni.

Schalke inaongoza badi ikiwa na pointi 50 baada ya kupoteza nao pointi 2 walipocheza na Hannover na kutoka sare ya bao 1:1.Bremen imeridhika na sare ya jana na kuondoka na pointi 1 ilioiwezesha kunyatia nafasi ya pili nyuma ya viongozi Schalke.

Kwa pointi hiyo 1, kocha wa Bremen alielezea kuridhika kwake namna hivi:

“Kuna mapambano mengi ambamo tulicheza uzuri sana na kutamba ,lakini mwishoe tuliondoka uwanjani mikono mitupu.Leo tunaondoka na pointi 1 na yafaa kuridhika.”

Nae beki mshahara wa timu ya Taifa na mlinzi wa wa Bayern Munich,Philip Lahm, akisikitishwa kupoteza jana pointi 2 kwa Bremen alisema:

“Tumepoteza leo pointi2,hatahivyo, nadhani tumecheza uzuri kabisa na ulikua mmoja ya michezo yetu maridadi kabisa ikiwa sio ndio bora kabisa.Matokeo lakini ndio si ya kuridhisha.”

Na huko Afrika Mashariki: Young Africans ya Tanzania inajinoa kwa changamoto ya mwishoni mwa wiki ijayo ya kombe la klabu bingwa barani Afrika kati yake na Petro Atletico ya Angola. Katika duru ya kwanza ,Younga iliizaba Petro mabao 3:0.

Nchini Kenya, dimba limetoka korokoroni na Kenya sasa ni ruhusa kucheza dimba la kimataifa-yasema FIFA-shirikisho la dimba ulimwenguni-uamuzi ambao umekaribishwa nchini Kenya na KFF-shirikisho la dimba .

Tukigeukia robo-finali ya Kombe la FA la Uingereza,Chelsea ilitoka nyuma kwa vishindo na baada ya kuchapwa mabao 2 na mwishoe ikasawazisha mabao 3-3 na Tottenham Hotsopur hapo jana.Alikua Salomon Kalou alietia bao la dakika ya mwisho kusawazisha.

Blackburn Rovers ilikuwa timu ya kwanza kukata tiketi ya nusu-finali baada ya kuikumta Manchester City mabao 2:0.Watford ikajiunga nao pale ilipowika mbele ya Playmouth Argyle kwa bao 1:0.

Bao la dakika ya mwisho alilotia mamadou Niang liliikokoa Olympique Marseille kutoka suluhu bao 1:1 na viongozi wa ligi Olympique Lyon jana.

FC Barcelona ya Spain,waliovuliwa taji la ubingwa wa ulaya wiki iliopita wanamshukuru sana chipukizi wa Argentina, Lionel Messi kwa kupiga hodi mara 3 langoni mwa Real Madrid na kuitikiwa karibu katika sare ya mabao 3:3 ya mahasimu hao wakubwa wa dimba nchini Spian.Messi alitia mabao yote 3 ya Barcelona.