1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern Munich yamkaribisha Pep Guardiola

25 Juni 2013

Baada ya kuwa majini kwa mwaka mmoja, hatimaye Josep “Pep” Guardiola ameibuka na kukaribishwa rasmi kama kocha wa Bayern Munich. Guardiola amesema ni Bayern iliyomtafuta

https://p.dw.com/p/18vEz
Sportdirektor Matthias Sammer (l-r), Trainer Pep Guardiola, der Vorstandsvorsitzende Karl-Heinz Rummenigge und Präsident Uli Hoeneß kommen am 24.06.2013 zur Vorstellung Guardiolas als neuer Trainer des Fußball-Bundesligisten FC Bayern München während der Pressekonferenz in der Allianz Arena in München (Bayern) auf dem Podium. Foto: Peter Kneffel/dpa
Deutschland Fußball FC Bayern München Vorstellung Trainer GuardiolaPicha: picture-alliance/dpa

Guardiola amesema leo kuwa aliamua kujiunga na washindi hao wa mataji matatu msimu huu kwa sababu ya wachezaji na historia ya kujivunia ya klabu hiyo. Mhispania huyo mwenye umri wa miaka 42, amewaambia waandishi wa habari kwamba alihitaji changamoto mpya baada ya misimu minne yenye mafanikio kama kocha wa Barcelona kipindi ambacho alishinda mataji 14, ikiwa ni pamoja na mataji mawili ya Champions League, kati ya mwaka wa 2008 – 2012. kisha akaamua kupumzika kwa mwaka mmoja jijini New York pamoja na familia yake ambako alianza kujifunza Kijerumani na akasaini mkataba wa miaka mitatu na Bayern, ambao walinyakua taji la Bundesliga, Kombe la Shirikisho pamoja na Champions League chini ya Jupp Heynckes katika msimu uliopita.

Pep azungumza Kijerumani

Guadiola alianza kwa kusema na namnukuu, “niwie radhi kwa kijerumani changu, New York siyo sehemu nzuri ya kujifunza Kijerumani”. Akizungumza katika lugha ya Kijerumani, Kocha huyo amesema anahisi kama amepewa zawadi na ana furaha kujiunga na Bayern.

Jupp Heynckes amemwachia Pep Guardiola kazi kubwa
Jupp Heynckes amemwachia Pep Guardiola kazi kubwaPicha: picture-alliance/dpa

Amesema yuko tayari kufanya kila awezalo kuendeleza mafanikio ya klabu ya Bayern kwa kuiweka katika kiwango cha juu alichoweka mtangulizi wake Jupp Heynckes.

Mwenyekiti wa klabu hiyo Karl-Heinz Rummenige amesema ni bahati, fahari na mafanikio kumpata kocha mwenye ufansi kote ulimwenguni. Kwamba pande zote zilitaka hilo: Bayern ilimtaka Pep, na Pep akaitaka Bayern. Hivyo ni hadhithi ya kusisimua ya Bayern Munich na soka ya Ujerumani.

Matarajio yako juu. Bayern wamehamishia mazoezi yao ya siku mbili chini ya Guardiola katika uwanja wa Allianz Arena huku takribani mashabiki 25,000 wakitarajiwa kushuhudia. Mengi yameandikwa kuhusiana na filosofia ya mchezo wa kasi wa Tiki Taka ambao Barcelona waliutawala chini ya Mhispania huyo, lakini itasubiriwa kuona kama atahama kutoka muundo wa 4-2-3-1 hadi 4-3-3.

Mwandishi: Bruce Amani/reuters/DPA

Mhariri: Yusuf Saumu