1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern wapata kionjo kabla ya Champions League

13 Mei 2013

Bayern Munich, walipata kionjo cha kile watakachokishuhudia pale watakaposhinda kombe la Ligi ya Mabingwa barani Ulaya, wakati maelfu ya mashabiki walipojitokeza kusheherekea taji lao la 23 la Bundesliga

https://p.dw.com/p/18Wzn
Bayern Munich supporters wait for the Bayern team with the German soccer championship trophy during a reception at Munich's townhall May 11, 2013. Bayern held their 23rd German league title on Saturday after a comfortable 3-0 over Augsburg as they prepare for the all-German Champions League final against Borussia Dortmund in two weeks. REUTERS/Michaela Rehle (GERMANY - Tags: SPORT SOCCER)
FC Bayern München Meisterfeier MarienplatzPicha: Reuters

Na sasa miamba hao wa soka Ujerumani wanatumai kuwa shehere hizo ni kionjo tu cha kile kitakachofanyika wakati watakapopambana na mahasimu wao wakali wa Bundesliga Borussia Dortmund katika fainali ya Champions League uwanjani Wembley mnamo Mei 25.

Baada ya kunyanyua taji la Bundeliga, kufuatia ushindi wao wa magoli matatu kwa sifuri dhidi ya Augsburg katika uwanja wa Allianz Arena, Bayern sasa wameyaangazia macho fainali ya Champions League huku wakitaraji kushinda mataji matatu msimu huu. Mnamo Juni mosi watacheza fainali ya Kombe la Shirikisho Ujerumani DfB Pokal dhidi ya VfB Stuttgart mjini Berlin.

Jupp Heynckes aliwaaga mashabiki wa nyumbani
Jupp Heynckes aliwaaga mashabiki wa nyumbaniPicha: Getty Images

Pep Guardiola kuchukua usukani

Kocha Jupp Heynckes ambaye anamwachia usukani Pep Guardiola, aliwaaga mashabiki baada ya kunyanyua taji katika mechi yake ya mwisho nyumbani kama kocha. Wiki ijayo, Bayern watachuana na Borussia Moenchengladbach. Bayern wana pointi 88 kileleni mwa ligi, huku Dortmund ambao walitoka sare ya magoli matatu kwa matatu na Wolsfburg wakifuata na pointi 66. Leverkusen wako katika nafasi ya tatu na pointi 62 na tayari wamejikatia tikiti ya kucheza ligi ya mabingwa.

Jumamosi ijayo ambayo ndio itakuwa siku ya mwisho ya msimu itashuhudia vita vikali vya kuwania nafasi ya nne, na mechi ya mchujo ya kufuzu katika Champions League kati ya Schalke 04 na nambari tano Freiburg. Schalke, baada ya kumpa kaimu kocha wake Jens Keller mkataba wa miaka miwili, iliteleza kwa kufungwa mabao mawili kwa moja nyumbani na VfB Stuttgart, wakati Freiburg ikitoka nyuma na kuishinda Greuther Furth mabao mawili kwa moja.

Ushindi huo ulitosha kuwahakikishia Freiburg tikiti ya kucheza Europa League, na kuwazuia SV Hamburg, lakini sasa pia wanaweza kupata nafasi ya kufuzu katika Champions League. Atakayeshinda nyumbani kwa Freiburg, atamaliza wan ne wakati sare pia ikiipa fursa Eintracht Frankfurt. Kama Frankfurt watawashinda Wolfsburg basi watawapa kibali cha kucheza Europa League.. Hamburg watstahili kuwachapa Leverkusen nyumbani na waombe matokeo mengine yawaendee ili wacheze Europa Legaue, wakati Moenhengladbach wakiwa na nafasi ndogo sana ya kucheza Ulaya.

Schalke 04 walionyesha shukrani kwa kumpa mkataba wa miaka miwili mkufunzi wao Jens Keller
Schalke 04 walionyesha shukrani kwa kumpa mkataba wa miaka miwili mkufunzi wao Jens KellerPicha: picture-alliance/dpa

Werder Bremen wanusurika

Katika upande wa chini wa ligi, Werder Bremen waliondoka katika eneo la kushushwa daraja na kuwaacha Fortuna Düsseldorf, Augsburg na Hoffenheim wakiendelea na mapambano ya kukwepa shoka la kushushwa daraja. Hoffenheim ambao waliduwazwa mabao manne kwa moja nyumbani kwa Hamburg, na lazima washinde dhidi ya Dortmund, wanaonekana kuanguka pamoja na Greuther Furth ambao tayari waliiaga Bundesliga. Augsburg na Düsseldorf, ambazo zina pointi mbili mbele ya Hoffenheim, zinaonekana kuwa timu zitakazokutana katika mchujo wa kupandishwa daraja, wakati Augsburg itakapoialika Fürth nayo Düsseldorf ikicheza nyumbani kwa Hanover.

Kwingineko sherehe zimeendelea mwishoni mwa wiki wakati ligi tofauti zikifikia tamati ya msimu. Barcelona walinyanuya taji lao la 22 la La Liga na la nne katika miaka mitano iliyopita. Hii ni baada ya nambari mbili Real Madrid kutoka sare ya goli moja kwa moja na Espanyol.

Sir Alex Ferguson aliwataka mashabiki na wachezaji kusimama na kocha mpya David Moyes
Sir Alex Ferguson aliwataka mashabiki na wachezaji kusimama na kocha mpya David MoyesPicha: PAUL ELLIS/AFP/Getty Images

Mkufunzi Jose Mourinho alichezesha kikosi dhaifu huku akiiangazia macho fainali ya Ijumaa ya kombe la mfalme dhidi ya Atletico Madrid na nafasi yao ya mwisho ya kumaliza msimu na taji. Barca walisajili ushindi wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Atletico Madrid. The Catalans wana pointi 91, Madrid pointi 81 nao Atletico na 72. Valencia wako katika nafasi ya nne na 59 baada ya ushindi wao wa magoli manne kwa sifuri dhidi ya Real Vallecano

PSG washeherekea ushindi

Nchini Ufaransa, Paris St Germain wamenyakua taji lao la kwanza la Ligue 1 tangu mwaka wa 1994 kwa ushindi wa goli moja kwa sifuri dhidi ya Olympique Lyon, ambao uliwasongeza pointi saba mbele ya Olympique Marseille zikiwa zimesalia mechi mbili msimu ukikamilika. Ushindi wa Marseille wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Toulouse uliwapa tikiti ya kucheza katika ligi ya mabingwa Ulaya msimu ujao. Lyon wamechukua nafasi ya tatu na ya mwisho ya kucheza Champions League.

Kule England, Manchester United walimuaga Sir Alex Ferguson kwa ushindi wa mchuano wa mwisho wa nyumbani baada ya kuifunga Swansea magoli mawili kwa moja. Ferguson amewataka wachezaji na mashabiki wa United kusimama pamoja na mkufunzi wao mpya David Moyes, ambaye pia klabu yake anayoiaga ilipata ushindi wa mabao mawili kwa sifuri dhidi ya Fulham katika uwanja wa Goodison Park. Hata hivyo vita vya kumaliza katika nafasi ya nne vitapamba moto wakati Arsenal itakapokutana na Wigan kesho Jumanne. Tottenham Hotspurs iliwashinda Stoke City mabao mawili kwa moja na kuruka hadi nafasi ya nne mbele ya Arsenal. Chelsea ambao wako katika nafasi ya tatu waliwazidi nguvu Aston Villa kwa kuwafunga magoli mawili kwa moja.

Mwandishi: Bruce Amani/DPA/Reuters/AFP

Mhariri: Yusuf Saumu