1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern yamtafuta kocha mpya baada ya kumtimua Kovac

Bruce Amani
4 Novemba 2019

Schalke ilitoka nyuma mara mbili na kuibwaga Augsburg, na Fortuna Dusseldorf ikashinda Rheine Derby ya Bundesliga, katika siku ambayo ilitawaliwa na habari za Bayern Munich kuwachana na kocha Niko Kovac.

https://p.dw.com/p/3SRMS
FC Bayern München - Niko Kovac
Picha: picture-alliance/SvenSimon/F. Hoermann

Bayern imesema jana kuwa iliamua kumuachia Kovac mwenye umri wa miaka 48 baada ya timu hiyo kupata kipigo kikubwa kabisa kwenye ligi katika zaidi ya miaka 10. Mabao 5 – 1 dhidi ya timu yake ya zamani Eintracht Frankfurt Jumamosi. Mwenyekiti Karl-Heinz Rummenigge amesema mchezo wa timu katika wiki za karibuni na matokeo waliyopata vimeonyesha kuwa kulikuwa na haja ya kuchukua hatua.

Kichapo cha Jumamosi kiliiacha Bayern na pengo la pointi nne nyuma ya vinara Borrusia Moenchengladbach katika Bundesliga. Msaidizi wa Kovac, kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Ujeurmani Hansi Flick, amechukua mikoba ya kuiongoza Bayern kwa muda. Na ili kujua mengi zaidi kuhusu habari hiyo, nina mwenzangu hapa kutoka dawati la michezo Sekione Kitojo. Kitojo uamuzi wa Bayern ulikushangaza?

Schalke baada ya ushindi mgumu wa 3 -2 dhidi ya Augsburg wako katika nafasi ya sita katika upande wa juu wa ligi ambao nambari mbili Borussia Dortmund na namba tisa Hoffenheim wanatenganishwa na pointi mbili tu, nyuma ya Gladbach ambao wako kileleni na mwanya wa pointi tatu.

Augsburg wako katika nafasi ya tatu kutoka mkiani pointi sawa na nambari mbili kutoka nyuma Cologne ambao walipoteza 2 – 0 katika derby dhidi ya watani wao Fortuna Dusseldorf kwa mara ya kwanza katika miaka 36.