1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern yatengana na kocha Carlo Ancelotti

Sekione Kitojo
29 Septemba 2017

Bayern Munich itaanza maisha mapya baada ya kutengana na kocha wake mkuu Carlo Ancelotti jana Alhamis(28.09.2017), wakati kocha wa mpito Willy Sagnol anachukua hatamu kabla ya mchezo wa Jumapili dhidi ya Hertha Berlin.

https://p.dw.com/p/2kwnM
FC Bayern Muenchen- Carlo Ancelotti
Picha: Imago/Sven Simon/F. Hoermann

Mabingwa  wa  Bundesliga  Bayern Munich  walidhalilishwa  kwa  kipigo  cha  mabao 3-0 dhidi  ya  paris saint-Germain  katika  mchezo  wa  pili  wa  makundi  wa  Champions League siku  ya  jumatano, na  klabu  hiyo  ilichukua  hatua  za  haraka  kumfuta kazi kocha Ancelotti siku  ya  Alhamis.

Fußball Champions League - Paris St. Germain - FALSCHES CINEMASCOPE
Kocha wa zamani wa Bayern Munich Carlo AncelottiPicha: picture-alliance/Laci Perenyi

Baada  ya  kubugia kipigo  cha  mabo 2-0 dhidi  ya  Hoffenheim  na  kuachia ushindi wakati wakiongoza  kwa  mabao 2-0 nyumbani  dhidi  ya  VFL Wolfsburg, hata kiwango cha Bayern katika  Bundesliga  kilikuwa  mbali  na chake cha kawaida cha udhibiti katika  wiki  za  hivi karibuni.

Wakati  klabu  hiyo  imebakia  katika nafasi ya tatu  nyuma  ya  Hoffenheim  na  viongozi Borussia  Dortmund , minong'ono  ya  kutokuwa  na  amani  ndani  chumba  cha  kuvalia wachezaji  iliongeza  mbinyo  kwa  Anceloti.

Champions League - Paris Saint Germain vs FC Bayern München- Carlo Ancelotti und Willy Sagnol
Kocha wa Bayern Ancelotti(kushoto) akiwa na msaidizi wake Willy Sagnol (katikati)Picha: picture-alliance/DPPI Media/J. M. Hervio

Akikabiliwa  na  ukosoaji  kutoka  kwa  mashabiki  na  vyombo  vya  habari  kwa  kushindwa kumtumia  vizuri Thomas Mueller , uhusiano  wa Ancelotti na  wachezaji  kama  Robert Lewandowski, Arjen Robben  na  frank Ribery pia  unaripotiwa  kuwa  uliathirika.

Wakati  Sagnol  anachukua  hatamu  za  uongozi  kwa  muda, Bayern itabidi  kuimarisha msimu  wake wakati  wanasafiri  kwenda  kupambana  na  Hertha  Berlin.

Kikosi cha Carlo Ancelotti

Ancelotti alikosolewa  vikali kwa  jinsi  alivyoteua  kikosi  chake  kilichopambana  na  PSG, na Mats Hummels , Robben, Ribery  na  Jerome Boateng wanatarajiwa  kurejea  katika  kikosi cha  kwanza  dhidi  ya  Hertha.

Fußball Champions League/ Ribery FC Bayern München-RSC Anderlecht 3-0
Frank Ribery akitupa jezi yake kwa hasiraPicha: picture-alliance/SvenSimon/F. Hoermann

"Natarajia  maendeleo  chanya  kutoka  katika  timu, na  bila  shaka  nia  ya  kucheza  vizuri," amesema  bosi  wa  klabu  hiyo Karl_heinz Rummenigge  baada  ya  kutupwa  nje  Carlo Ancelotti.

Bayern inahitaji  kocha  mpya  wa  muda  mrefu, na  kuna fununu  kwamba  baada  ya mapunziko ya  michezo  ya  timu  ya  taifa  viongozi watafikia  uamuzi wa  kumleta  mmoja kati  ya  makocha  ambao  wanazungumziwa  sana  kumrithi Carlo Ancelotti.

Champions League - Borussia Dortmund v AS Monaco - Thomas Tuchel
Aliyekuwa kocha wa zamani wa Borussia Dortmund Thomas Tuchel Picha: picture-alliance/Digitalfoto Matthias

Majina yanayotajwa  kuchukua  nafasi  hiyo  ni  pamoja  na  kocha  wa  hivi  sasa  wa  TSG Hoffenheim , Julian Nagelsmann , na Thomas Tuchel  kocha  wa  zamani  wa  Borussia Dortmund. 

Tatizo  la  nagelsmann  ni  kwamba  bado  ana  mkataba  na  Hoffenheim, lakini  Thomas Tuchel  hana  kazi  kwa  sasa  na  anaweza  kupatikana  mara  moja.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afpe