1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bei za Hisa zilishuka Ulaya Ijumaa asubuhi

Kalyango Siraj10 Oktoba 2008

Vigogo wa fedha kutoka mataifa saba duniani wakutana Marekani

https://p.dw.com/p/FXsM
' Maamawe'. Mtaalam Justin Bohan aonekana kama kusema baada ya bei za hisa kuporomoka katika soko la New YorkPicha: AP

Mgogoro wa kifedha ulioikumba sekta hii ya Marekani baado unaendelea licha ya juhudi za benki kuu na serikali duniani kuupatia ufumbuzi.Uingiliaji huo haujazaa matunda yaliyolengwa na pia umeshindwa kuzuia kuporomoka kwa mosoko ya hisa duniani.

Hali hiyo imepelekea shirika la fedha duniani –IMF kusema kuwa mgogoro wa kifedha wa Marekani unatishia kusababisha kudorora kwa uchumi wa dunia nzima.

Hali ya kuendelea kwa mgogoro huo kumesababisha mawaziri wa fedha kutoka katika kundi linaloitwa la mataifa saba kuwa na kikao cha dharura mjini Washington Ijuma.

Mkutano huo unawakusanya pamoja mawaziri wa fedha pamoja na wakuu wa benki kuu za mataifa ya Marekani, Ujerumani, Japan, Ufaransa, Uingereza ,Italy na Kanada.

Rais Bush amekubali kukutana na mawaziri wa fedha wa kundi hilo kesho jumamosi.

Aidha mgogoro huo umesababisha kuendelea kuporomoka kwa masoko ya hisa duniani. Soko la Hisa la Dow Jones la viwanda lilipoteza point karibu 600 alhamisi na kwenda chini ya kiwango cha 9,000, kwa mara ya kwanza tangu agosti mwaka wa 2003.Siku kama hii, mwaka mmoja uliopita, soko la Dow Jones lilisherehekea kufikia alama ya juu ya pointi 14,000. Masoko yote ya Faharasa ya Ulaya yalifunga kazi jana yakiwa katika hasara. Yeye Meneja mkurugenzi wa IMF Dominique Srauss-Kahn, akiwa mjini Washington amesema kuwa mgogoro huu wa kifedha unaweza tu kutatuliwa kupitia juhudi za ushirikiano wa kimataifa.

Mwenyekiti wa mataifa nane tajiri duniani-G8- waziri mkuu wa Japan Taro Aso,amesema leo kuwa ataitisha kikao cha dharura ikiwa wakuu wa fedha wanaokutana mjini Washington hawatafikia suluhisho la mgogoro huu wa kifedha.

Mataifa hayo ya G8 ni Uingereza, Kanada, Ufaransa, Ujerumani, Italy, Japan, Urusi na Marekani.Viongozi wa mataifa hayo walikuwa na kikao chao cha kila mwaka kaskazini mwa Japan mwezi Julai.

Viongozi wawili wa chama cha Democratic katika baraza la Congress la Marekani wamemtaka rais Bush kuitisha mkutano wa mataifa ya G8 ili kutafuta ufumbuzi wa mgogoro huo.Viongozi hao wametoa taarifa ikisema kuwa raia wa Marekani pamoja na wadunia nzima wanaikodolea macho Marekani ili kutoa mwongozo.

Yeye Barack Obama anaepigania kwenda Ikulu ya Marekani akitumia tiketi ya chama cha Democratic, ameonya dhidi ya alichokiita hofu miongoni mwa wananchi na kuwaomba watulie, huku akitoa mwito wa kupata ufumbuzi wa haraka wa mgogoro huo wa kifedha ambao unaikumba dunia ,baada ya kuanzia Marekani.

Serikali ya Marekani ilitoa dola billioni 700 ili kusaidia kumalizika kwa mgogoro huo lakini hadi sasa mambo hayajatengamaa.

Hisa za Ulaya zimeshuka leo Ijumaa kwa kiasi cha asili mia 10 wakati wa kufunguliwa soko la hisa la faharasa la Umoja wa Ulaya. Kabla ya kufikia asili mia 10 hisa zilikuwa zimeshuka chini hadi asili mia 8 kiwango cha chini sana kuwahi kufikiwa tangu Julai 2003. Katika soko la hisa la Japan la NIKKEI hisa zilishuka hadi asili mia 10 leo Ijumaa.

Na nchini Urusi,Ijumaa bunge la nchi hiyo la Duma limepasisha mipango miwili ya serikali yenye nia ya kuunusu mfumo wa fedha wa nchi hiyo.Mpango huo ni wa dola billioni 86 ambazo zitatumiwa na na benki ama makampuni ambayo yatahitaji msada wa mtaji.

Kutokana na hali hii Meneja Mkurugenzi wa IMF Srauss-Kahn amesema kuwa ahueni kutokana na mgogoro huu itaweza kupatikana katikati au baadae mwaka ujao wa 2009.