1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Benazir Bhutto auwawa kwa kupigwa risasi

28 Desemba 2007
https://p.dw.com/p/ChHL

ISLAMABAD

Waziri Mkuu wa zamani wa Pakistan Benazir Bhutto ameuwawa kwa kupigwa risasi kufuatia mkutano wa hadhara wa kampeni ya uchaguzi katika mji wa Rawalpindi hapo jana.

Msemaji wa chama chake cha PPP amesema mtu aliekuwa na silaha alimfyetulia risasi Bhutto mara mbili wakati akiwa kwenye gari lake akiondoka kwenye mkutano huo.Mtu huyo baadae alijiripuwa katikati ya wafuasi wa Bhutto na kuuwa takriban watu 20 na kujeruhi wengine wengi.

Mwili wa marehemu Bhutto tayari umesafirishwa kupelekwa kwenye jimbo la kusini la Sindh kwa mazishi ambapo anatarajiwa kuzikwa kwenye makaburi ya familia pembezoni mwa kaburi la baba yake waziri mkuu wa kwanza wa Pakistan kuchaguliwa na wananchi Zulfikar Ali Bhutto ambaye alipinduliwa na jeshi hapo mwaka 1977 na baadae kunyongwa.

Viongozi mbali mbali duniani wameelezea kufadhaishwa kwao na kulaani vikali mauaji ya Bhutto akiwemo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki- moon

Ban anatowa wito kwa serikali ya Pakistan kuwafikisha mbele ya sheria wahusika wa mauaji hayo na anaalani kwa nguvu zote mauaji ya Benazir Bhutto.

Baruwa pepe iliotolewa na kituo cha televisheni cha Marekani cha CNN imeonyesha Bhutto akimlaumu Rais Pervez Mushrraf kwa kushindwa kumpatia ulinzi katika miezi tete kabla ya kuuwawa kwake.

Rais Musharraf ametangaza siku tatu za maombolezo ya taifa na ametowa wito wa kuwepo kwa utulivu huku kukiwepo na ghasia katika miji kadhaa ambapo imeripotiwa watu kadhaa wameuwawa.

Waziri Mkuu wa zamani na kiongozi wa upinzani Nawaz Sharif ametowa wito wa kufanyika kwa mgomo wa taifa leo hii na kususiwa kwa uchaguzi wa bunge uliopangwa kufanyika tarehe nane Januari.