1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Benjamin Netanyahu akabiliwa na shinikizo kubwa

Zainab Aziz Mhariri Saumu Yusuf
1 Machi 2019

Mwanasheria mkuu wa serikali nchini Israel anakusudia kumfungulia Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu mashtaka ya rushwa, udanganyifu na kuvunja uaminifu pia anadaiwa kupokea zawadi kutoka kwa mfanyabiashara tajiri.  

https://p.dw.com/p/3EKLb
Israel Premierminister Benjamin Netanjahu
Picha: picture-alliance/newscom/D. Hill

Akijibu madai hayo, Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amesema kwenye televisheni kwamba kesi inayomkabili itasambaratika kama gunia tupu. Wakati zimebakia wiki chache kabla ya kufanyika uchaguzi, Netanyahu amesisitiza kuwa kesi hiyo ni njama za wanasiasa wa mrengo wa kushoto za kumwandama kwa lengo la kuiangusha serikali yake.

Mwanasheria mkuu wa Israel, Avichai Mandelblit ametangaza uamuzi wa kumshtaki Netanyahu kabla ya uchaguzi huo utakaofanyika wa tarehe tisa April ambapo wachambuzi wanasema Netanyahu atakabiliwa na ushindani mkali wa muungano wa kisiasa wa mrengo wa wastani unaongozwa na aliyekuwa mkuu wa majeshi wa Israel Benny Gantz.

Bwana Gantz kiongozi wa mfungamano wa vyama vya mrengo wa wastani na atakayekuwa mshindani mkuu wa Netanyhu katika uchaguzi wa mwezi ujao alisema hayo alipokutana na waandishi wa habari baada ya mwanasheria mkuu kutangaza nia ya kumfikisha mahakamani waziri mkuu huyo kwamba chama chake asilani hakitashirikiana na Netanyahu katika serikali ya mseto baada ya uchaguzi. 

Kiongozi wa mfungamano wa vyama vya mrengo wa wastani nchini Israel Benny Gantz
Kiongozi wa mfungamano wa vyama vya mrengo wa wastani nchini Israel Benny GantzPicha: DW/T. Kraemer

Kwa mujibu wa mwanasheria mkuu, bwana Netanyahu atajibu mashtaka juu ya kupokea zawadi za bei kubwa ikiwa pamoja na sigara ,pombe na vito vya thamani  vinavyikadiriwa kufikia bei ya dola 264,100.Anatuhumiwa kupokea zawadi  hizo kutoka  kwa mkurugenzzi  wa filamu wa Hollywood Arnon Milchan na kutoka kwa tajiri  mkubwa kutoka Australia Kames Packer. Hata hivyo waziri mkuu huyo halazimiki kisheria kujiuzulu endapo atafunguliwa mashtaka lakini itabidi afanye hivyo ikiwa atahukumiwa baada ya rufani zote kuwasilishwa. Hata hivyo washirika wa Netanyahu katika serikali ya mseto wameamua kusimama pamoja na waziri mkuu huyo, licha ya uamuzi wa mwanasheria mkuu. Wamesema kwamba waziri mkuu huyo hawezi kutiwa hatiani mpaka hapo itakapothitishwa mahakamani. 

Vyama vya upinzani vimepania kuendelea kumshinikiza waziri mkuu Netanyahu hadi siku ya  uchaguzi. Chama cha mrengo wa kushoto kinapanga kuitisha maandamano makubwa mwishoni mwa wiki hii mjini Tel Aviv. Waandamanaji kwa mara nyingine watamtaka Netanyahu ajiuzulu na watamkumbusha kwamba mnamo mwaka 2008 yeye alimtaka waziri mkuu wa wakati huo Ehud Olmert ajiuzulu alipokabiliwa na  mashtaka. Uchaguzi wa Israel unatarajiwa kufanyika tarehe 9 april huku mabadiliko mengi yakitarajiwa kati ya sasa na wakati huo wa uchaguzi.

Vyanzo: AFP/AP/DPA