1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BERLIN: Merkel atafuta maafikiano kuhusu Katiba ya Umoja wa Ulaya

17 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBr0

Kansela wa Ujerumani,Angela Merkel hii leo anakutana na Waziri mkuu Mirek Topolanek wa Jamhuri ya Czech,karibu na mji wa Berlin.Mkutano huo ni sehemu ya juhudi zake za kutafuta maafikiano kuhusu mkataba wa katiba ya Umoja wa Ulaya uliokwama.Baadae leo hii pia Merkel ataelekea Luxembourg,kuonana na Waziri Mkuu Jean-Claude Juncker.Merkel,anatumani kupata masikilizano kuhusu mkataba huo wa katiba,kabla ya mkutano wa kilele wa Umoja wa Ulaya utakaofanywa mjini Brussels juma lijalo.Mgogoro uliopo,ni dai la Poland la kutaka mfumo wa kupiga kura katika umoja huo ubadilishwe kwa manufaa ya madola madogo na ya wastani.Siku ya Jumamosi, Merkel alikutana na Rais Lech Kaczynski wa Poland na inasemekana kuwa viongozi hao hawakuweza kuafikiana.Ujerumani hivi sasa,imeshika wadhifa wa urais unaozunguka kila miezi sita,katika Umoja wa Ulaya.Katiba ya Umoja wa Ulaya imekwama tangu wapiga kura nchini Ufaransa na Uholanzi kuikataa katiba hiyo,katika kura ya maoni iliyopigwa miaka miwili iliyopita.