1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Biden kupigia jeki mikakati ya Marekani Afghanistan.

Munira Mohammad/AFP9 Machi 2009

Wiki moja tu baada ya Marekani, kugusia sera zake mpya Afghanistan, Makamu wa rais Joe Biden kutilia mkazo zaidi ushirikiano huu na mataifa ya NATO.

https://p.dw.com/p/H8b2
Makamu wa rais wa Marekani Joe BidenPicha: AP


Kwanza ilikuwa Hillary Clinton na sasa ziara ya Joe Biden, mjini Brussels inaangaziwa na wachanganuzi kama harakati za msukumo wa kurekebisha sera za kivita za Marekani katika mataifa kama Afghanistan na Pakistan.


Utakumbuka kuwa kampeini ya rais wa Marekani Barack Obama ilituwama katika kufuata mkondo tofauti na mtangulizi wake George Bush. Biden atakuwa anazidisha nguvu tu ushirikiano wa Marekani na mataifa wanachama wa NATO baada ya vidokezo ni ipi sura mpya ya Marekani kama ilivyoonyeshwa na waziri wake wa mambo ya nje Hillary Clinton alipokutana na mawaziri wa mambo ya nje wa Jumuiya ya NATO:



'' Hii ni ishara kuwa utawala wa Obama una nia hasa ya kukabiliana na hali ilivyo nchini Afghanistan, na kwamba serikali hii mpya imetambua kuwa hatua watakayoichukua Afghanistan itachangia pakubwa kuirudishia Marekani hadhi yake mbele ya macho ya ulimwengu.'' Ni matamshi ya afisa mmoja wa ngazi za juu wa utawala wa Obama.


Mwandishi wa gazeti la New York Times, Sheryl Stolberg alinukuliwa akisema jitihada hizi mpya za Marekani ni mchakato wa sera zake mpya ya kukabiliana na mahasimu wao wa jadi.


OTON, US OFFICIAL


''Nadhani tunashuhudia jinsi rais Obama anabadili sera za Marekani katika kukabiliana na mahasimu wetu, katika kila njia. Umeona Iran ikipewa mualiko kuchangia katika kupata suluhu Afghanistan, mbali na kuinyoshea mkono Syria, hii ni muhimu.''


Biden atafanya mazungumzo na baraza kuu la jumuiya ya NATO linaloshughulika na maswala ya kisiasa na maamuzi kwa mataifa hayo 26 wanachama wa jumuiya hiyo. Pia atakaa mezani na katibu mkuu wa NATO Jaap de Hoop Scheffer pamoja na maafisa wakuu wa serikali ya mwenyeji wake Ubelgiji.


Obama ameendeleza kampeni ya kuikagua sera mpya ya kivita nchini Afghanistan na mapambano dhidi ya wenye siasa kali na hali tete nchini Pakistan tangu alipoingia madarakani mapema mwaka huu.


Tarehe 3 mwezi Aprili rais Obama atahudhuria mkutano wake wa kwanza wa mataifa shirika wa jumuiya ya NATO hivyo anatazamia kuwa amejihami na muongozo mpya wa vipi Marekani imekagua sera zake za kivita. Mshauri wake wa maswala ya usalama James Jones anatazamiwa amemuandaa Obama vilivyo kabla ya safari yake ya kwanza Ulaya, ambapo pia atahudhuria mkutano wa nchi 20 zilizoendelea kiuchumi na kongamano la Umoja wa Ulaya mjini Prague katika jamhuri ya Cheki.


Ishara ya kwanza kuwa serikali ya Obama imebadili mambo nchini Afghanistan ni pale rais huyo wa Marekani alipoagiza kutumwa kwa kikosi cha wanajeshi wengine 17,000- kwani hali ya kiusalama ilikuwa inazorota nchini humo. Kamanda wa jeshi la Marekani nchini Afghanistan Jenerali David McKiernan alikuwa ameonya kuwa mambo yanakwenda mrama na alihitaji vikosi zaidi kama tayari wanajeshi 30,000.


Obama tayari ameahidi kuwa ataondoa majeshi ya Marekani nchini Iraq ifikapo Agosti mwaka 2010 ili kuondoa mzigo mkubwa unaobebwa na Marekani na pia kuelekeza makali yao ya kijeshi nchini Afganistan wanaohitaji msaada wa dharura. Katika mahojiano na gazeti la New York Times Obama alikiri kuwa Marekani imezidiwa na vita Afghanistan na kugusia huenda Marekani ikajaribu kuanzisha majadiliano na makundi yenye siasa ya wastani ya Taliban.


Kasi hii ya Marekani kuhusu Afghanistan iliibua hisia kuwa huenda rais Obama akatumia tajriba yake Ulaya kuzishawishi nchi shirika za NATO kutuma wanajeshi zaidi Afghanistan au kushurutisha nchi zingine kuondoa vikwazo wanajeshi wao watashiriki katika vita maeneo gani- lakini tayari nchi kadhaa za NATO zimetoa wazi misimamo yao kuwa haziwezi kutuma vikosi zaidi Afghanistan.


Afisa mmoja wa Marekani amenukuliwa akisema Biden atawasilisha ujumbe mahsusi kwa nchi wanachama wa NATO kuwa serikali ya Obama inahitaji msada na mchango wao huku ikijibidisha kukagua sera zake Afghanistan.