1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Boateng kuondoka Bayern mwishoni mwa msimu

8 Aprili 2021

Bayern Munich imethibitisha kuwa Jerome Boateng, mwenye umri wa miaka 32 ataondoka klabuni humo baada ya mkataba wake kukamilika mwishoni mwa msimu huu, japo tangazo hilo limesababisha mvutano ndani ya klabu hiyo.

https://p.dw.com/p/3rjBG
UEFA Champions League -  Group A - Fußball - RB Salzburg vs. FC Bayern München
Picha: Andreas Schaad/AP/dpa/picture alliance

Bayern Munich imethibitisha kuwa Jerome Boateng, mwenye umri wa miaka 32 ataondoka klabuni humo baada ya mkataba wake kukamilika mwishoni mwa msimu huu, japo tangazo hilo limesababisha mvutano ndani ya klabu hiyo.

Mabingwa hao watetezi wa ligi kuu ya kandanda ya Ujerumani, Bundesliga tayari wamemsajili Dayot Upamecano, mwenye umri wa miaka 22 kutoka kwa mahasimu wao RB Leipzig, lakini atajiunga na miamba hao kuanzia msimu ujao.

"Huo ulikuwa uamuzi wa pamoja wa usimamizi wa klabu na kocha pia alihusika”, mkurugenzi wa Bayern Munich Hasan Salihamidzic aliliambia shirika la habari la Sky. "Tayari nilimueleza Boateng juu ya uamuzi huu, na ameelewa.”

Boateng alifanya kosa na kuruhusu bao la ushindi la Paris Saint Germain katika mechi ya jana Jumanne ya mchuano wa ligi ya mabingwa Champions League.

Ushindi wa PSG wa 3-2 ulivunja rekodi ya Bayern Munich kwenda mechi 19 bila kupoteza katika michuano hiyo ya Ulaya, na kutia guu moja ndani ya nusu fainali.

Boateng, alionekana kuzidiwa maarifa na mshambuliaji wa PSG Kylian Mbappe mwenye umri wa miaka 22 aliyefunga mabao mawili katika uwanja wa Allianz Arena.

Mechi ya marudiano itachezwa Jumanne ijayo mjini Paris.

Boateng anajiunga na David Alaba, ambaye pia ataondoka Bayern mwishoni mwa msimu huu. Hata hivyo, tofauti na Alaba aliyekataa kusaini kandarasi mpya, Boateng hakupewa ofa hiyo.

Tangu ajiunge na Bayern akitokea Manchester City mnamo mwaka 2011, Boateng ameshinda ligi ya mabingwa mara mbili na ligi ya Bundesliga mara nane.