1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Borussia Dortmund bado iko kileleni, Bayern yaja

Sekione Kitojo
3 Desemba 2018

Dortmund yaongeza  kasi, Bayern yaanza tena  kushinda, timu zinazoiwinda Borussia Dortmund  kileleni  zateleza.

https://p.dw.com/p/39Mc7
1. Bundesliga | Borussia Dortmund v SC Freiburg | Torjubel (2:0)
Kikosi cha Borussia Dortmund Picha: Reuters/L. Kuegeler

Borussia  Dortmund  imefungua  mwanya  wa  pointi 7  kati  yake  na timu  inayoifuatia  katika  nafasi  ya  pili  Borussia Moenchengladbach , baada  ya  kuizaba  SC  Freiburg  kwa  mabao 2-0  na  Gladbach  kuteleza  mbele  ya  RB Leipzig  kwa  kupandikwa mabao 2-0.  Leipzig  imesogea  juu  na  kuchukua  nafasi  ya  tatu ikiwa  na  pointi 25 , moja  nyuma  ya  Gladbach.

1. Bundesliga | Werder Bremen v Bayern München | Torjubel (1:2)
Wachezaji wa Bayern Munich wakifurahia bao dhidi ya Werder BremenPicha: Imago/foto2press

Bayern Munich nayo  ikasogea  hadi  nafasi  ya  nne  kutoka  nafasi  ya  tano  pale ilipoishinda  Werder Bremen  kwa  mabao 2-1 katika  mpambano mkali  siku  ya  Jumamosi.

Bayern Munich  imesogea  na  kufika katika  nafasi ya  kucheza  katika  Champions  League  msimu  ujao, lakini  inafukuzwa kwa  karibu  na  Eintracht  Frankfurt  iliyosalia  na pointi 23  baada  ya  hapo  jana  Jumapili  kusalimu  amri  mbele  ya Wolfsburg  kwa  kukandikwa  mabao 2-1 na Wolfsburg  kutua  katika nafasi  ya  8  ikiwa  na  pointi 18 kutokana  na  michezo 13  ya Bundesliga.

Fußball Bundesliga 1899 Hoffenheim vs Schalke 04 | Jubel
Wachezaji wa Hoffenheim wakifurahia bao dhidi ya Schalke 04Picha: picture-alliance/dpa/U. Anspach

Hoffenheim  ilitosheka  na  sare  ya  bao 1-1  dhidi  ya  Schalke 04, timu  ambayo  itajipima  nguvu  na  viongozi  wa  ligi  na  mahasimu wao  wakubwa Borussia  Dortmund  katika  mchezo  wa  14  wa Bundesliga mwishoni mwa juma hili.  Leo  hii  Jumatatu  Bundesliga  inaendelea , wakati Nuernberg  inaikaribisha  Bayer  Leverkusen  katika  mchezo  wa mwisho  wa  13  katika  Bundesliga.

 

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afpe / dpae / rtre / ape

Mhariri: Mohammed Khelef