1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bouteflika ambadilisha meneja wake wa kampeni ya urais

Sekione Kitojo
3 Machi 2019

Rais wa Algeria Abdelaziz Bouteflika amembadilisha meneja wake wa kampeni kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa Aprili ambapo anatarajiwa  kuwania muhula wa tano madarakani,shirika la habari la APS limesema Jumamosi(02.03.2019).

https://p.dw.com/p/3ENK6
Algerien | Präsident Abdelaziz Bouteflika
Picha: Reuters/R. Boudina

 

Taarifa  za  uteuzi wa  Abdelghani Zaalane  zimekuja  siku  moja baada  ya  mamia  kwa  maelfu ya  Walgeria  kuandamana  dhidi  ya muhula  mwingine  wa  urais  kwa  kiongozi  huyo mwenye  umri  wa miaka 82, ambaye  yuko  nchini  Uswisi kwa  ukaguzi  wa  afya yake. Zaalane  ni  waziri.

Algerien Proteste gegen die Regierung
Maandamano ya kuipinga serikali na hatua ya kuwania kuchaguliwa tena kuwa rais BouteflikaPicha: AFP/R. Kramdi

Shirika  la  habari  la  APS halikutoa  sababu  yoyote kuhusiana  na uamuzi  huo  wa  Bouteflika kumbadilisha  meneja  wake  wa  hapo mwanzo Abdelmalek Sellal , ambaye  alisema  siku  ya  Jumanne kuwa  rais  atawasilisha  nyaraka  zake  rasmi  za  uchaguzi  leo Jumapili, muda  wa  mwisho  wa  kufanya hivyo kwa  wagombea.

Wapinzani  wanasema  Bouteflika , ambaye  aliugua  kiharusi nmwaka  2013 na  ameonekana  hadharani  mara  chache  tangu wakati  huo, hawezi  tena  kuliongoza  taifa  hilo  la  Afrika  kaskazini, mtoaji  mkubwa  wa  mafuta  na  gesi.

Lakini  katika  ishara  ya  udhaifu  kuweza  kutoa  changamoto  ya kupambana  dhidi  ya  chama  tawal  cha  National Liberation Front FNL, muungano  wa  kundi  la  vyama  vya  upinzani kwa  mara nyingine  tena  umemtaka  Bouteflika  kujiondoa lakini  kundi  hilo halijamteua mgombea wao.

Siku  ya  Ijumaa  kulishuhudiwa  kujitokeza  kwa  kundi  kubwa kabisa  kuwahi  kuonekana  la  maandamano  makubwa  nchini Algeria  linalopinga  serikali  tangu  vuguvugu  la  maandamano  ya umma  katika  mataifa  ya  Kiarabu  miaka  minane  iliyopita. Bouteflika  hajazungumzia  moja  kwa  moja  maandamano  hayo.

Algier, Algerien Gewaltsame Proteste gegen die Regierung
Waandamanaji wakipambana na polisi mjini AlgiersPicha: Reuters/Z. Bendemra

Mpiganaji  mkongwe

Kama  wengi  wa  watu  mashuhuri  katika  nchi  hiyo  iliyotoa viongozi  wa  FNL, maafisa  wa  jeshi  na  wafanyabiashara  matajiri, Bouteflika ni mpiganaji  mkongwe wa  vita  vya  kuwania  uhuru nchini  Algeria  dhidi  ya  Ufaransa   kuanzia  mwaka  1954-1962. Amekuwa  madarakani  tangu mwaka  1999.

Maafisa  walisema  wiki  iliyopita  kwamba  atakwenda  Geneva kwa kile  ambacho  hakikuwekwa  wazi  kuhusu  uchunguzi  wa  afya yake.

Vyombo  vya  habari  nchini  Algeria  havikuripoti  kuhusu  safari yake lakini televisheni  ya  umma  ya  Uswisi  imesema  jioni  ya Jumamosi kwamba  Bouteflika ameendelea  kuwapo  katika  hospitali ya  chuo  kikuu  mjini  Geneva.

Jumla  ya  watu 183 walijeruhiwa  katika  maandamano  ya  Ijumaa nchini  Algeria na  mtu  mmoja  amefariki  kutokana  na  mshituko  wa moyo, limesema  shirika  la  habari  la  APS.

Mji  mkuu  Algiers  ulikuwa  kimya  jana  Jumamosi  na  maduka yalifunguliwa.

Maandamano  makubwa, ambayo  ni  nadra  kuyaona  nchini  Algeria huku  kukiwa  na  ulinzi  mkali, dhidi  ya   hatua  ya  kuchaguliwa  tena kwa  Bouteflika yalianza  wiki  moja  iliyopita na  yameongezeka idadi ya  washiriki.

Algerien Proteste gegen die Regierung
Vijana wameingia mitaani kupinga rais Bouteflika kuwania kuchaguliwa tenaPicha: picture-alliance/dpa/A. Belghoul

Wengi  wa  Waalgeria  wameepuka  harakati  za  wazi  za  kisiasa kwa  miaka  kadhaa, wakihofia  matatizo  kutoka  jeshi  la  usalama ama kuchoshwa  na viongozi  wa  vita  vya  ukombozi  ambao wameendelea  kuiongoza  nchi  hiyo  tangu  uhuru.

Baada  ya  mapigano  ya  muongo  mmoja  ya  kundi  la  Kiislamu ambayo Bouteflika  aliyazima  mapema  katika  utawala  wake, Waalgeria  mara  kadhaa  wamevumilia  mfumo  wa  kisiasa unaokandamiza  upinzani kama  gharama wanayolipa kwa  ajili  ya amani  na  uthabiti.

Mwandishi: Sekione Kitojo / rtre

Mhariri: Jacob Safari Bomani