1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Brazil yaiangusha Chile kupitia penalti

29 Juni 2014

Chile walikuwa karibu kuwasababishie wenyeji Brazil maafa. Lakini Selecao walinusurika baada ya bahati kuwaendea katika mikwaju ya penalti na kuingia robo fainali ya Kombe la Dunia ambapo watambana na Colombia

https://p.dw.com/p/1CSB3
WM 2014 Achtelfinale Brasilien Chile
Picha: Francois Xavier Marit/AFP/Getty Iamges

Baada ya kuponea katika Kundi D pamoja na Uholanzi na Uhispania, Chile ilionekana kuwa timu inayoweza kusababisha usumbufu sana dhidi ya mpinzani yeyote, na ilitarajiwa kuwaangusha wenyeji Brazil. Lakini Selecao walianza mechi huku wakifyatua riasasi moto moto ili kuwaonyesha La Roja kuwa matumaini yoyote ya kuwaangamiza yangegonga ukuta.

WM 2014 Achtelfinale Brasilien Chile
Mlinda lango wa Brazil Julio Ceaser alifanya kazi ya ziadaPicha: Reuters

Brazil ilikuwa imekosolewa kwa kukosa mshikamano kwenye timu pamoja na mkakati, lakini washambuliaji wa Brazil Neyamar, Hulk na Fred – kila mara walikuwa wanawasumbua mabeki watatu wa Chile. Selecao walichanganya pasi ndefu na fupi kwa wakati mmoja na kuwaacha wapinzani wao wakihema mjini Belo Horizonte.

Ukurasa wa magoli ulifungulwia hata hivyo, katika dakika ya 18. Neymar aliichonga Freekick, ambayo ilipigwa kichwa na Thiago Silva, na Gonzalo Jara akafunga goli katika lango lake. Hakukuwa na mbinu nyingine ambayo Jara angetumia – David Luiz alikuwa nyuma yake na angeweza kufunga kwa urahisi.

Brazil iliendeela kutengeneza nafasi, lakini ilikuwa zamu ya La Roja kusawazisha katika dakika ya 32. Hulk aliupoteza mpira, na Alexis SANCHEZ akawa tayari kumalizia mambo. Goli hilo halikutarajiwa, lakini lilimkumbusha kila mmoja katika uwanja wa Estadio Mineiro kuwa Chile wanaweza kuwa wapinzani hatari sana.

Katika kipindi cha pili, Chile ilirekebisha makosa yao katika safu ya ulinzi na kuanza kuumiliki mpira na kutengeneza nafasi kadhaa za kufunga magoli. Katika dakika ya 55, Hulk aliupata mpira na akafunga goli, lakini likakataliwa baada ya refa kuamua kuwa aliunawa makusudi, na akapewa kadi ya njano badala ya jina lake kuwa kwenye orodha ya waliofunga magoli.

WM 2014 Achtelfinale Brasilien Chile
Wachezaji wa Chile walizidiwa na uchungu baada ya mechiPicha: Reuters

Dakika 90 zilikamilika mambo yakiwa 1-1. Dakika 30 za ziada hazikuwa na nafasi za kufunga magoli, kwa sababu wachezaji walikuwa wamechoka miguu. Lakini Mauricio Pinilla nusra awape ushindi Uruguay lakini kombora lake lilikuwa juu kidogo tu..milimita kadhaa na likaugonga mwamba wa lango na kurudi uwanjani.

Ukafika wasaa wa mikwaju ya penalti, na baada ya penalti nne kila timu, mambo yakawa 2-2. Neymar alijitokeza, na akamwbaga kipa Bravo. Jara akajipa ujasiri kupiga penalti ya Uruguay, lakini akakosea na mpira ukaugonga mlingoti. Hivyo Brazil walifuzu baada ya ushindi wa magoli 4-3 kupitia penalty na kuliondolea taifa zima jinamizi. Chile wamerudi nyumbani wakifahamu kuwa walichungulia hatua ya robo fainali na nusra waweke historia.

Mwandishi: Bruce Amani/DW/DPA/AFP
Mhariri: Sekione Kitojo